BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

Polisi aeleza alivyokuta misokoto nyumbani kwa Wema



Tokeo la picha la wema sepetu 
Dar es Salaam. Inspekta Msaidizi wa Polisi Wille ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jinsi alivyopekua nyumba ya msanii wa filamu, Wema Sepetu  na kubaini misokoto inayodhaniwa kuwa ni ya bangi.
Wema na wenzake Angelina Msigwa na Matrida Abbas wanakabiliwa na mashtaka mawili ya kupatikana na misokoto ya bangi.
Inspekta Wille (43) kutoka Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Kanda Maalumu ya Dar es Salaam ambaye ni shahidi wa pili wa upande wa mashtaka amedai hayo leo Jumanne akitoa ushahidi mahakamani.
Akiongozwa na Wakili wa Serikali, Costantine Kakula mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba amedai Februari 4 alipewa kazi na mkuu wake ya kufanya upekuzi nyumbani kwa Wema.
Amedai aliongozana na askari wa kike Mary, Koplo Robert, Konstebo Hassan na dereva kuelekea Ununio anapoishi Wema ili kufanya upekuzi.
Shahidi alidai walipofika waligonga mlango na walipokewa na wasichana wawili. Pia, waliomba mjumbe wa nyumba kumi aitwe na alifika Steven Noho.
Alidai walimweleza wamekwenda nyumbani kwa Wema kufanya upekuzi na wanatafuta dawa za kulevya na kitu chochote ambacho wangekitilia shaka.
“Wema alisema dada yake awepo ili ashuhudie upekuzi huo, dada yake alifika na tukapekua. Upekuzi wetu ulianzia jikoni juu ya kabati la vyombo, tulikuta msokoto mmoja unaodhaniwa kuwa ni wa bangi na karatasi ya kusokotea,” amedai shahidi huyo.
Amedai, “Tulielekea katika chumba cha Wema ambacho anahifadhia nguo na vitu vyake vingine, mlango ulikuwa umefungwa. Wafanyakazi wake walituletea ufunguo tukafungua na kukuta vipisi na msokoto unaodhaniwa kuwa ni bangi dirishani.”
Shahidi amedai upekuzi uliendelea katika chumba cha wasichana wa kazi wa Wema ambako walikuta kiberiti ambacho ndani kilikuwa na msokoto ambao ulionekana umeshavutwa.
Amedai baada ya upekuzi, walisaini hati ya ukamataji mali ambapo aliisaini yeye,  Wema, wafanyakazi wake, dada yake, na mjumbe wa eneo la Ununio. Shahidi alidai walienda kituoni ambako walimkabidhi vielelezo Robert.
Amedai Februari 8 yeye na askari Mary walimpeleka Wema katika ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kipimo cha mkojo. Alisema pia waliongozana na dada yake Wema.
Inspekta Wille amedai waliwasilisha fomu ya maombi ya kuwasilisha sampuli ya mkojo kwa mkemia Elias Mulima.
Amedai mkemia huyo alimpatia kifaa cha kuwekea sampuli hiyo askari Mary aliyefuatana na Wema sehemu waliyoelekezwa kwenda kutoa sampuli ya mkojo .
Shahidi amedai baada ya kutolewa sampuli hiyo, Mary aliikabidhi kwa mkemia Mulima kwa ajili ya uchunguzi.
Alidai sampuli hiyo iliwasilishwa kwa fomu ya maombi ambayo aliisaini pamoja na mkemia. Alipoonyeshwa fomu hiyo mahakamani aliitambua na akaomba kuitoa kama kielelezo cha ushahidi.
Wakili Peter Kibatala kwa niaba ya mawakili wenzake Jeremiah Mtobesya, Hekima Mwesigwa na Hassan Kihangio alipinga fomu hiyo kupokewa na Mahakama kama kielelezo akidai haijakidhi vigezo vya sheria.
Kutokana na pingamizi hilo, Wakili wa Serikali Kakula aliomba apewe muda. Hakimu ameahirisha kesi hadi leo saa tano asubuhi.Mwananchi
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: