BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

DENI LA TAIFA SASA LAFIKIA SH27 TRILIONI, KAULI YA SERIKALI YANENA KUWA TANZANIA INAKOPESHEKA.

Waziri wa Fedha na Uchumi, Saada Mkuya.

DAR ES SALAAM

LICHA ya deni la taifa kuongezeka na kufikia Sh27 trilioni mwaka jana, Serikali imesema bado ina sifa za kuendelea kukopa kutokana na mapato ya ndani kuwa madogo.


Akizungumza Dar es Salaam jana, Waziri wa Fedha na Uchumi, Saada Mkuya alisema jambo linalozingatiwa na Serikali ni kuhakikisha fedha za mikopo zinatumika kwa shughuli za kukuza uchumi.


“Deni la taifa linajumuisha deni la Serikali kutoka vyanzo vyake vya mapato ya ndani na nje ya nchi pamoja na deni la nje ambalo Serikali imelidhamini kwa sekta binafsi,” alisema Mkuya.


Alisema hadi kufikia Desemba mwaka jana, deni la taifa lilifikia Sh27 trilioni, kati ya kiwango hicho deni la nje ni Sh20.2 trilioni na ndani ni Sh6.8 1 trilioni, huku deni la nje la sekta binafsi likifika Sh3.5 trilioni.


“Tunaendelea kukopa na deni linaongezeka. Linaongezeka kwa mikopo inayochukuliwa na ile ambayo haijalipwa,” alisema.


Akitaja sababu za kuongezeka kwa deni hilo alisema: “Linaongezeka kwakuwa nchi bado inaendelea kukopa, kuendelea kuwepo kwa madeni ya nyuma kutokana na muda wake wa kuyalipa kutofika, kuongezeka kwa watu na shughuli za kiuchumi pamoja na kuwepo kwa madeni ambayo kwa mujibu wa mikataba yanatakiwa kusamehewa.”


Alisema kutokana na kuwepo kwa orodha ndefu ya nchi zinazokopa, hivi sasa Tanzania imejikita zaidi katika kukopa mikopo yenye masharti ya kibiashara ambayo ni tofauti na mikopo yenye masharti nafuu.


Hata hivyo, Mkuya alisema kila mwaka Serikali inafanya tathmini kama inaweza kuhimili deni kutokana na shughuli za kiuchumi ndani ya nchi. “Tathmini ya mwisho tumefanya Septemba mwaka jana, haifanywi na Serikali pekee, inahusisha pia Shirika la Kimataifa la Fedha (IMF) na Benki ya Dunia (WB),” alisema Mkuya.


Waziri huyo alivitaja viashiria vinavyoonyesha kuwa nchi ina uwezo wa kuhimili deni kuwa ni thamani ya deni la nje ikilinganishwa na uchumi wa nchi (GDP),”


“Deni la nje sasa hivi ni asilimia 25 ambayo ni sawa na asilimia 24.8 ya uchumi wa nchi. Lakini ukomo wa kukopa kwa kutumia kiashiria hiki ni asilimia 50 ya deni, hivyo bado tuna vigezo vya kukopa maana tupo katika asilimia 24.”


Alisema thamani ya leo la deni lote la taifa kwa uchumi wa nchi ni asilimia 40.5 na kwamba ukomo wake ni asilimia 74.


“Lakini hilo halitufanyi kukopa zaidi, ila kutokana na hali ya uchumi tutakopa katika vyanzo nafuu,” alinena.MWAANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: