Pius Msekwa.
WAKATI mjadala wa uteuzi wa mawaziri ukiendelea kupamba moto nchini, makada wakongwe wa CCM, Pius Msekwa na Peter Kisumo wamesema Rais Jakaya Kikwete ndiye mwenye mamlaka ya kuteua na habanwi na chama, wala mtu yeyote.
Wamesema chama kinaweza kumshauri Rais kuhusu uteuzi, lakini hakiwezi kumbana atekeleze uteuzi wa mawaziri kinaowataka.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti
hili, Msekwa alisema mwenye mamlaka ya kufanya uteuzi wa mawaziri nchini
ni Rais Jakaya Kikwete peke yake.
“Uteuzi wa mawaziri ni kazi ya Rais na katika
hilo, hana ubia na mtu na ndiyo mfumo uliopo na unaeleweka na kila mtu
na unatumiwa na karibu nchi zote duniani,” alisema Msekwa ambaye ni
Makamu wa Mwenyekiti mstaafu wa CCM Tanzania Bara.
Msekwa ambaye pia amewahi kuwa Spika wa Bunge
alisema haoni tatizo la mfumo katika suala zima la utendaji kazi wa
Serikali na kusisitiza kuwa Rais mpaka anafikia hatua ya kumteua mtu ni
wazi kuwa anajua utendaji wake wa kazi.
Alipoulizwa kama haoni uteuzi wa Rais ni kinyume
na maagizo ya Kamati Kuu ya chama hicho alisema: “Mawaziri waliitwa
mbele ya kamati na kilichozungumzwa ndani ya kikao hicho mimi na wewe
hatujui, pengine walijieleza vizuri na ikaonekana kuwa hawana tatizo na
kuamua kuwarejesha bila kuwapa adhabu yoyote.”
Kisumo
Naye Kisumo ambaye ni Mdhamini wa CCM, alisema, Rais anaweza kutekeleza au kutokutekeleza uamuzi unaotolewa na chama chake.
Alisema: “Siyo kila linalosemwa na chama lazima
Rais alitekeleze, hapana, kwani sijapata kuona mahali popote duniani
Rais akatekeleza matakwa ya chama. Urais siyo chama.”
Aliongeza: “Kazi ya kubadili Serikali ni kazi ya
Rais, kama chama kimeona kuna mawaziri mizigo hicho ni chama, lakini
Rais anaweza kuteua yeyote anayeona anafaa.”
Alisema chama kinapotaka kusema au kutoa maoni
yake juu ya jambo lolote hakiombi kibali kwa Rais kutokana na majukumu
ya vyama vya siasa kuwa ni kuwatetea wananchi wake.
“Rais anapofanya mabadiliko yake ya Serikali, nje
wananchi wanaweza kusema huyu anafaa au huyu hafai, lakini hiyo ni kazi
ya Rais kuona kama wanafaa au hawafai.”MWANANCHI
0 comments:
Post a Comment