BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

MKURUGENZI WA KATIBA, SHERIA NA HAKI ZA BINADAMU ACHARANGWA MAPANGA BAADA YA KUVAMIWA NA MAJAMBAZI NYUMBANI KWAKE, ALAZWA KATIKA WODI MAALUM HOSPITALI YA TAIFA YA MUHIMBILI JIJINI DAR ES SALAAM.

DKT Jakaya Mrisho Kikwete na Mama Salma Kikwete na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi Mhe James na daktari wa zamu wakimwangalia Mjumbe wa Tume ya Katiba Dkt Sengondo Mvungi aliyelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kitengo cha Mifupa (MOI) leo Oktoba 3, 2013 kufuatia kujeruhiwa kwake na watu wanaosadikiwa ni majambazi usiku wa Jumamos Oktoba 2, 2013.PICHA NA IKULU.
 

DAR ES SALAAM. 
MJUMBE wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini, Dk Sengondo Mvungi amejeruhiwa usiku wa kuamkia jana, baada ya kukatwa kwa mapanga na watu wasiojulikana waliovamia nyumbani kwake Mpiji-Magohe, jijini Dar es Salaam.


Dk Mvungi, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Katiba, Sheria na Haki za Binadamu wa NCCR-Mageuzi aliwahishwa kwenye Taasisi ya Mifupa Hospitali ya Muhimbili (MOI), ambako amelazwa katika wodi maalumu huku hali yake ikiwa mbaya.

Taarifa kutoka kwa ndugu na watu waliomtembelea hospitalini hapo wanasema kwamba hali ya Dk Mvungi ni mbaya kwani alikuwa hawezi hata kuzungumza.

Akisimulia tukio hilo, dereva wa Dk Mvungi anayeitwa Emmanuel Ntaro, alisema akiwa nyumbani kwake majira ya saa 6:30 usiku, alisikia mlipuko mkubwa kisha zikasikika kelele zikitokea nyumbani kwa bosi wake.

“Nilifika na kukuta hajitambui, tukampeleka Hospitali ya Tumbi Kibaha mkoani Pwani alikopatiwa huduma ya kwanza kabla ya kumpeleka MOI ambako anaendelea kuchunguzwa na kupatiwa matibabu,” alieleza Ntaro.

Alisema kuwa watu wapatao sita, walivamia nyumbani kwa Dk Mvungi ambako baada ya kuvunja mlango na kuingia ndani, walimjeruhi kwa kutumia mapanga huku wakidai wapatiwe fedha. Watu hao walimsababishia majeraha usoni, kichwani na sehemu nyingine za mwili.

Akizungumza na Mwananchi jana, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema mbali na kupata matibabu MOI, pia walilazimika kumpeleka Hospitali ya Aga Khan kwa ajili ya vipimo zaidi katika mashine ya CT Scan kama walivyoshauriwa na madaktari wa zamu.

Mbatia alisema kuwa baada ya Dk Mvungi kufanyiwa kipimo hicho alirudishwa tena MOI kwa matibabu na uangalizi maalumu. “Hali yake inaanza kuimarika tofauti na nilivyomuona saa nne asubuhi, “ alisema Mbatia muda wa saa 12 jioni jana alipozungumza na gazeti hili.

Alisema kwamba pia watu waliohusika na tukio hilo waliiba kompyuta mpakato (laptop) pamoja na bastola ya Dk Mvungi.
Kamanda wa Mkoa wa kipolisi Kinondoni, Cammilius Wambura alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

“Kweli hilo ni tukio la kihalifu na sisi tunaendelea kulifanyia kazi. Tunawahakikishia Watanzania kuwa watu hao watapatikana na kufikishwa kwenye mkono wa kisheria,” alisema. MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: