BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

TUNAPOAJILI VYETI BADALA YA UJUZI NA MAARIFA: TUTAFIKA (2).

 

HOJA yangu kuu kwenye mada hii tangu wiki iliyopita ni kuhusu vyeti kama kigezo pekee cha kuajiri wafanyakazi. Wafanyakazi wengi wanashindwa kuleta tija kwenye taasisi zetu hasa za Serikali, kutokana na mtindo wa kuajiri vyeti badala ya ujuzi, maarifa na ubunifu.


Mathalan, Kwa sasa hata dereva anayebeba roho za watu kwa anatakiwa awe na vyeti vya kidato cha nne na vyeti vya udereva, hata kama hajui kuendesha gari na hana uzoefu wa kazi hiyo.

Kila siku Taifa linapoteza maelfu ya Watanzania kwa vifo vinavyotokana na ajali ya magari kutokana na dhambi hii kuendelea kutawala kwenye sekta ya ajira, kuajiri vyeti badala ya ujuzi, utalamu na maarifa.
Madereva wataendelea kuua Watanzania kwa sababu wanaajiriwa kwa vyeti vya kidato cha nne pasipo ujuzi. Na wengine wanaajiriwa kutokana na “vyeti mabosi (vimemo kutoka kwa viongozi wakubwa).

Huwa najiuliza unahitaji mtu wa kujenga daraja, cheti cha nini badala ya kumpeleka kwenye eneo la daraja ajenge? Unahitaji mtu wa kurekebisha umeme, cheti cha nini badala ya kumkabidhi eneo lenye hitilafu ili atengeneze? Unahitaji ofisa kilimo, cheti cha nini? mpeleke shambani aonyeshe ujuzi wake.

Mbona Wamachinga wanafanya biashara nzuri kila mahali nchini bila kuonyesha vyeti vya kuhitimu masomo ya biashara? Mbona babu na bibi zetu vijijini wanafuga ng’ombe kwa maelfu bila kuwa na cheti cha kuhitimu mafunzo ya ufugaji?

Kwanini kwenye ajira tunakusanya vyeti badala ya kukusanya ujuzi? Kwanini tunakusanya lundo la makaratasi badala ya kukusanya lundo la ubunifu na maarifa? Kwa nini tunakusanya A na GPA nzuri ofisini badala ya kukusanya uvumbuzi na ubunifu? Kwa nini tunalipa mishahara vyeti badala ya kulipa mishahara kazi, ujuzi, maarifa na jitihada za watu?

Ieleweke siku zote kuwa; nguvu inayoendeleza taasisi au Taifa lolote haiko kwenye idadi ya digrii na vyeti vya watu wake.

Maendeleo yote duniani yameletwa na maarifa, ujuzi, ubunifu, uvumbuzi, jitihada ya kazi na kujituma. Kila mwenye sifa hizi hata kama hajawahi kuingia darasani lazima awe na mafanikio.

Ushahidi tunao; wako babu zetu vijijini hawajui A wala B. Lakini wanajitosheleza kwenye mahitaji ya msingi na kubaki na ziada. Wachina wanaoingia nchini hawana vyeti lukuki kama tunavyodhani. Wana ujuzi na maarifa ndiyo maana wanaajirika kila mahali.

Nazipongeza taasisi na kampuni ambayo zilizositisha kuita vyeti kwenye usaili wa ajira. Wao wanaomba wasifu (CV) wa mwombaji kisha anaitwa kwenye usaili. Wamefanikiwa. Wanapata wafanyakazi wazuri kwa sababu hawana ulevi tena wa kukusanya vyeti kama ilivyo katika sekta ya utumishi wa umma ikiratibiwa na sekretariati ya ajira.

Kulundika vyeti lukuki vya wafanyakazi na mafaili makubwa hakuna tija kwa maendeleo. Kujaza wafanyakazi wenye digrii nyingi na diploma kibao hakuwezi kuleta tija ofisini. Vyeti havifanyi kazi. Kinachofanya kazi na kuleta tija kubwa ni maarifa, ujuzi na ubunifu. Kujituma, uvumbuzi na jitihada ya kufanya kazi kwa malengo. MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

1 comments:

AMINA said...

Yani kuanzia elimu jinsi vyiti vinavyopatikana ni utata na ajira pia utata. tena siku hizi hawaangalii hata vyiti wanaangalia nani wanamjua.