BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

MGOGORO MPYA WAIBUKA BUNGE LA KATIBA DODOMA.

Mwenyekiti wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Freeman Mbowe.

DODOMA. 
BAADHI ya wenyeviti wa Kamati za Bunge la Katiba wamezikataa taarifa za wajumbe walio wachache ambazo wanapaswa kuzisoma leo bungeni, hivyo kuwataka waziandike upya kwa madai kuwa hazijafuata taratibu katika uandishi na zimejaa lugha ya kuudhi.
Wakizungumza na mwandishi wetu jana, baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo, ambao wapo katika kundi la wachache, walisema wenyeviti hao, ambao wengi wao ni viongozi wa CCM, wamegoma kuzipokea taarifa zao ambazo walipewa wazisome leo bungeni.


Mwenyekiti wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Freeman Mbowe alisema kuwa, mgogoro huo umeibuka kutokana na wajumbe wa Bunge hilo, ambao wengi wao wanatoka CCM, kupuuza hoja ya awali ya kutaka maoni ya walio wachache wayasome wenyewe bungeni, badala yake wakalazimisha yasomwe na wenyeviti wa kamati wanaotoka kwenye kundi la walio wengi.


“Wameshtuka walipoziona hoja zetu, hawakutarajia hoja za walio wachache, kwani wao hawasomi kanuni na hoja zao, nyingi wamekaririshwa, hivyo hawawezi kuzitetea,” alisema Mbowe. Alisema hadi jana jioni kwenye kamati yake, kulikuwa na mgogoro juu ya maoni ya walio wachache kama ilivyokuwa kwenye kamati nyingine.


Mjumbe wa Ukawa, Tundu Lissu alisema kamwe hawatakubali taarifa za walio wachache kupunguzwa maneno na wenyeviti wa kamati kwani maoni hayo siyo yao, ni ya wengine.


“Hizi taarifa ni zetu hatutakubali waondoe hata neno moja, waling’ang’ania kuzisoma sasa lazima wasome maneno yote kama kanuni inavyosema, wakipuuza kesho (leo) bungeni hatutakubali,” alisema Lissu.


Mmoja wa wenyeviti wa kamati hizo, Paul Kimili alikiri kuwa katika kamati yake Namba 12, aliomba taarifa ya walio wachache kuandikwa kwa kufuata utaratibu na kupunguza lugha ambazo alisema siyo nzuri.


“Ni kweli kuna mgogoro, hizi taarifa za wachache kuna maneno mengine makali sana ya kuudhi, sasa kwangu nimewaomba warekebishe tu,” alisema Kimiti.


Mwenyekiti wa Kamati Namba Tatu, Dk Francis Michael naye alisema amewataka wajumbe wa kamati ya walio wachache kurekebisha taarifa yao, baada kuandika maneno ambayo yanahitaji ushahidi.


Huu uamuzi wa kuwataka warekebishe baadhi ya maneno siyo wangu, ni wa Kamati. Kwanza ni mjumbe gani analalamika? Kanuni zipo wazi anayepaswa kuzungumza na vyombo vya habari ni mwenyekiti pekee na mjumbe mwingine akitaka kuzungumza lazima apate idhini ya mwenyekiti,” alisema Dk Michael. 


Mwenyekiti wa Kamati Namba 9, Kidawa Hamis na Mwenyekiti wa Kamati Namba tano, Hamad Rashid ambao jana mchana walikabidhi taarifa za kamati zao kwa Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samia Suluhu Hassan walisema kuwa katika kamati zao washauriana vizuri na hakuna mgogoro.


“Mimi kamati yangu tulikaa na kujadiliana na wachache wana taarifa yao na wengi wanayo ya pamoja, tatizo ambalo lilikuwapo, utakuta wachache wameandika maneno mengi zaidi ya kurasa 50 na walio wengi wana maneno machache, hivyo hapo lazima kufikia maridhiano,” alisema Hamis.


Hata hivyo, Suluhu, alisema hadi jana, alikuwa hajapokea malalamiko ya kamati yoyote ya maoni ya walio wachache kukataliwa.MWANANCHI

Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: