BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

SHIRIKISHO LA VYMA VYA WAFANYAKAZI (TUCTA) LAJIVUA LAWAMA MADAI YA WALIMU.

https://hivisasa.co.tz/wp-content/uploads/2013/11/Nicholaus-Mgaya.jpg
SHIRIKISHO la Vyama vya Wafanya kazi (TUCTA) limesema kutokana na madai ya walimu yakiwamo malimbikizo ya fedha za likizo na kupandishwa madaraja kuwa ya muda mrefu, wameamua kila wilaya waende kudai wenyewe kwa wakurugenzi wao.

Shirikisho hilo limeeleza kuwa viongozi wanapokwenda kudai na kutoa kauli mbalimbali inaonekana kama wanataka umaarufu hivyo kuwataka walimu kudai wenyewe kwa wakurugenzi kwa njia wanazoona zinafaa.

Kauli imepingwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani aliyesema mpaka mwezi huu madai ya walimu kwa mishahara yamelipwa karibu yote na yaliyobaki ni moja moja ambayo waajiri walieleweshwa.

Alisema kwa sasa serikali inadaiwa Sh bilioni 10 za madeni mapya ambazo ni kwa ajili ya kupandishwa vyeo walimu na nyongeza za mwaka jana na zitaanza kulipwa mwezi huu huku akieleza kuwa matumizi mengine kama likizo, uhamisho na mengineyo yanafanywa na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi).

Akizungumza na gazeti hili jana, Katibu Mkuu wa Tucta, Nicholaus Mgaya alisema madai hayo yamekuwapo siku nyingi ila tatizo ni kwamba viongozi wanaolipa wana majibu ya kisiasa.

“Siku nyingi zimepita bila malipo hivyo naona kitendo cha walimu wa wilaya ya Kinondoni kuandamana kwa mkurugenzi ni sawa kwani sisi tukifuatilia sana tunaambiwa tunataka umaarufu, sasa tumeamua kutumia mtindo wa kila wilaya walimu kwenda kudai kwa mkurugenzi wao,”alisema.

Alitoa mfano kuwa wafanyakazi wa serikali za mitaa nao wanaidai serikali zaidi ya Sh bilioni 17 kwa muda mrefu, lakini wakurugenzi hawaweki fedha hizo kwenye bajeti ili malipo hayo yafanyike.

Alisema pia suala hilo la madai ya walimu wameliweka kwenye ajenda iwapo wataonana na Rais Jakaya Kikwete au Waziri Mkuu Mizengo Pinda na kueleza maagizo ya Rais hayakufanyiwa kazi.

Alisema walipokutana na Rais Kikwete mwaka jana, aliwaagiza wakurugenzi kuhakikisha malipo hayo yanalipwa haraka lakini wamekaidi. Aidha,Waziri Kombani alisema suala la madai yao ofisi yake ilifanya uhakiki na viongozi wa vyama vya walimu ambao wanapaswa kufuatilia mpaka kulipwa kwani wanawakata asilimia mbili ya mshahara kwa kazi hiyo hivyo wameshindwa kazi.

Alitaka viongozi hao kwenda wizarani na kuona madai ya walimu kwa kila wilaya yaliyopo katika mtandao na kuahidi kuwa deni hilo litalipwa mapema iwezekanavyo huku wakiwa na deni la zaidi ya Sh bilioni tatu ambalo linatakiwa kuhakikiwa.

Wakati serikali ya awamu ya nne inaingia madarakani deni la walimu lilikuwa Sh bilioni 90 na sasa limebaki chini ya Sh bilioni tatu. Alisema katika uhakiki walishirikiana na makatibu wa vyama vya wafanyakazi katika kila wilaya kutokana na kuwakata asilimia mbili za mishahara hivyo waendelee kuwahakikia.

Kombani alieleza kuwa kuna madeni ya wafanyakazi wa aina mbalimbali wakiwamo wahudumu wa afya na madaktari lakini yale ya walimu yamekuwa yakipewa kipaumbele kutokana na kuwa ni wengi hivyo ni vyema kuwa na subira.

Pia, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba aliwatoa hofu walimu kuwa serikali itahakikisha katika mipango yake inamaliza madeni yote yaliyokwisha hakikiwa kwani nia ya serikali iko wazi kutokana na malipo hayo yanavyopungua kila mwaka.

Aliwataka wanaodai kwenda kwa waajiri wao kuhakikiwa na kuangalia kama madeni wanayoona wanadai kweli yanatambuliwa na serikali ili kuwa na uhakika na kwa yale ambayo hayajahakikiwa kupeleka vielelezo.

Walimu wa shule za msingi na sekondari wilayani Kinondoni walivamia katika ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa hiyo juzi, wakidai stahiki zao na utatuzi wa matatizo sugu yakiwamo malimbikizo ya mishahara, posho za safari, likizo na kupandishwa madaraja.

Kabla ya kwenda kwa ofisi ya mkurugenzi, walianza msafara wa madai katika ofisi ya Chama cha Walimu ya (CWT) Kinondoni na kuelezwa na viongozi wa CWT kuwa, wamekuwa wakiyawasilisha manispaa madeni yao bila utekelezaji hivyo waliamua kwenda ofisini kwa Mkurugenzi wa manispaa ya Kinondoni, Mussa Natty kutaka utekelezaji.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: