BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

MASWALI MENGI NA MAGUMU MAUAJI WA ASKARI POLISI NA VIONGOZI WA CCM PWANI


Mkazi wa Kitongoji cha Kazamoyo wilayani Rufiji, Maimuna Nyingilini akiwa na watoto wake nje ya nyumba yao. Maimuna ni mmoja wa wanawake waliopoteza waume zao kutokana na mauaji ya mkoani Pwani.

Dar es Salaam.
Mfululizo wa mauaji ya viongozi wa serikali za mtaa katika maeneo kadhaa ya mkoani Pwani yameacha maswali mengi ambayo hayajajibiwa.

Wananchi wanaoathirika moja kwa moja na hali ya kukosekana usalama, wanaamini au kuhofia kuwa mamlaka zimeshindwa kuyapatia majibu haraka.

Ni kwa nini mamlaka hazitoi taarifa kuhusu maendeleo ya uchunguzi wa chanzo na sababu za mauaji hayo? Je, kuna haja ya kutangaza hali ya hatari katika maeneo yaliyoathirika? Je, uwepo mkubwa wa askari katika maeneo husika unasaidia kukomesha mauaji? Wauaji ni akina nani na ni nini sababu ya kufanya hivyo? Je, polisi wameshindwa au kuna haja ya kupeleka wanajeshi sasa?

Hayo ni baadhi ya maswali ambayo wafuatiliaji wa mambo na wananchi wanatamani kupata majibu yake.

Tayari watu zaidi ya 32 wameshauawa katika maeneo hayo tangu Januari 2015 wakati mauaji hayo yalipoanza kuripotiwa kwa uzito na vyombo vya habari nchini.

Mbunge mmoja kutoka eneo lililoathirika na mauaji hayo ambaye aliomba asitajwe jina kwa usalama wake, amesema kwa hali ilivyo sasa mamlaka za ulinzi na usalama zinapaswa kutoa taarifa za maendeleo ya uchunguzi ili kuondoa karaha kubwa kwa wananchi.

“Walau sasa polisi wana dalili za kubadili mbinu. Walilivamia suala hili kichwakichwa bila kuwa na taarifa za uhakika. Sasa wanaonekana wamekusanya taaarifa kuhusu genge la wauaji. Bila shaka wauaji watamalizwa siku za hivi karibuni,” alisema mbunge huyo.

Anasema hakuna haja ya kuleta majeshi mengine kuwapa nguvu polisi, wala kutangaza hali ya hatari kwa sababu hali hiyo haijawa tishio.

Katika kile kinachoonekana kuwa makubaliano ya kutolizungumzia suala la mauaji Pwani, mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Ernest Mangu, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Bulimba hawataki kuzungumzia suala hili.

Mbunge mwingine wa eneo hilo amezungumza na Mwananchi kwa njia ya simu na kuonyesha kutawaliwa na hofu ya mauaji kiasi cha kukosa kabisa imani hata na mwandishi. Anasema amelazimika kubadilili kabisa mfumo wake wa maisha kwa ajili ya usalama wake.

“Huwezi kujua nani anafuatia kuuawa. Inaweza kuwa mimi. Siwezi kukuamini hata wewe kwa sababu siwezi kuthibitisha wewe ni mwandishi kwa maongezi ya simu. Unaweza kuwa mmoja wa wale wauaji na unapanga kuniua,” alisema mbunge huyo akiwa Dodoma anakohudhuria kikao cha Bunge la Bajeti.

“Mambo ni zaidi ya unavyodhani kaka. Huwezi kuamini hivi tunavyoongea natetemeka,” alisema.

“Leo hii nalazimika kufanya siri hata sehemu ninayokuwa wakati wa usiku. Hata mke wangu hajui nalala wapi. Hili ni genge hatari wanaoweza kumfuata mtu yeyote na mahali popote ndani ya nchi hii.”

Diwani wa CCM katika moja ya maeneo yaliyoathirika na mauaji, anatoa maoni yanayoshabihiana na mbunge huyo.

Diwani huyo anajutia aumuzi wake wa kuchukua fomu na kugombea nafasi hiyo ya uongozi katika Uchaguzi wa Mwaka 2015.

“Nia yangu ilikuwa ni kutoa mchango wangu kwa maendeleo ya nchi yangu lakini mambo yamekuwa tofauti na nilivyoamini,” alisema. “Hivi sasa tunaongoza watu ambao hawako huru kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kuhofia usalama wao. Ni afadhali hata nisingegombea nafasi hii.”Mwananchi
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: