BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

WATOTO WACHANGA WANAOZALIWA NA JINSIA MBILI NAMNA WALIVYO KWENYE MISUKOSUKO YA KUUAWAWA

NI simulizi ya miaka mitano iliyopita, lakini ina uhai hadi sasa. Mume na mke nchini Kenya walizaa watoto na katika mazingira ya kutatanisha, mume alimtaka mke amuue mtoto mara tu baada ya kujifungua. Kisa? Eti mila inasema ‘ni mkosi.’

Mke hakukubali. Alimhamishia mtoto mafichoni na kumhadaa mume kwamba alishamuua.

Wakati hilo linatokea, Zainab ambaye ni mkunga wa jadi aliyemzalisha mtoto huyo, anaeleza mshangao wake kwamba amekuwa anasimamia watoto kujifungua kwa miaka mingi, lakini safari hiyo imekuwa na utata mkubwa kwake.

Zainab anasema kuna mambo tata anayofanyiwa wanapozaliwa watoto kuhusu jinsia ya mtoto, kama ni ama mvulana au msichana, kwa namna kitovu kilichezewa kabla ya kukatwa.

Anasema uzoefu wake wa ‘miaka nenda – rudi,’ daima hajawahi kutambua ilikosimamia jinsia ya mzaliwa huyo.

“Hata nikijaribu kuangalia kama ni mvulana au msichana, naona inanichanganya tu. ‘Kachanga’ haka kana sehemu ya kike na kiume,” anafafanua.

Mkunga huyo anasema kutokana na hilo linavyomchanganya, huwa anapomkabidhi mtoto hasemi kama ni wa kiume au wa kike, kama alivyozoea kwa familia zingine.

Anasema, kuna jambo linalowashangaza, kwamba wakati mke anakuwa ametatanishwa mno na kilichotokea, baba wa mtoto anakuwa katika hali fulani ya kutokuwa na shaka juu ya kilichotokea.

Hoja ya baba hiyo inaelezwa katika kauli ya nukuu yake akitamka:“Hatuwezi kumpeleka mtoto huyu nyumbani ni wa kuuawa tu.”
Mama huyo anapinga hoja kwa kauli: “Mtoto huyu kaumbwa na Mungu, halafu anauawa!’

Baadaye alitamka: “Yeye (mume) anasisitiza na ninaishia kumwambia mwache mtoto nibaki naye. Nitaenda kukuulia. Lakini sikumuua, bali nilimficha.”

Mke huyo ambaye bado yuko na mumewe, anasema alikuwa na tabia ya kufuatilia kwa kumvizia kuona kama mtoto yupo au la, lakini mke alimsisitizia kwamba, alishamuua.

MKUNGA ARITHI MTOTO
"Mwaka mmoja baadaye, mzazi huyo (wa kiume) alipata habari kuwa mtoto wao yuko hai na wakaja kuniona,” anasema mkunga Zainab

“Wakaniambia (wazazi) kamwe usitoe habari kuwa mtoto ni wao. Nilikubali na tangu hapo nimekuwa nikimlea mtoto peke yangu.

Ni hatari isiyo ya kawaida,” anaongeza.

Katika jamii ya mkunga Zainab na nyinginezo nchini Kenya, zinaamini kuwa na mtoto mwenye jinsia mbili ni ‘mkosi’ kwao, unaowaletea laana hadi majirani.

Hivyo, kitendo cha mkunga Zainab kumchukua mtoto kuwa wake, alijibebesha balaa ambalo naye aliamua kuwa tayari kupambana nalo.

Nwaka 2012, ikiwa miaka miwili baadaye, Zainab alipatwa na mshangao kuzalisha tena mtoto mwenye jinsia mbili, kutoka kwa mama yule yule.

"Safari hii, mzazi hakunitaka nimuue mtoto, bali niliomba nitoroke nikiwa na mtoto. Wazazi hawakunitaka nimuue mtoto. Mama naye alikuwa peke yake na akakimbia na kuniachia mtoto mchanga,” anasema Zainab.

Kwa mara nyingine mkunga alilazimika kumchukua mtoto kwenda kumlea nyumbani kwake, lakini mume alilalama kutokana na linalotokea, kwamba linaleta mkosi katika jamii.

"Kila alipoenda kuvua samaki, aliambulia wachache na akashutumu ‘mikosi’ hiyo kuwa inatokana na watoto," anasema Zainab, jambo analosema alipata shaka juu ya tabia ya mumewe na akaamua kutoroka na watoto wale.

"Ulikuwa uamuzi mgumu, kwani nilikuwa na maisha mazuri nikiwa na mume wangu. Tumelea watoto pamoja, hadi wajukuu. Lakini huwezi kuishi katika mazingira hayo ya vitisho na ugomvi. Nililazimika kutoroka."

"Alisema ni kwa sababu (watoto) wametuletea mkosi. Alipendekeza nimpatie watoto ili awatumbukize mtoni,” anasimulia Zainab na kuongeza: “Nilikataa na kumwambia sitoliruhusu hilo litokee. Alikuwa mkali na tangu hapo tukawa tunapigana kila mara.”

Zainab anasema kutokana na hilo, aliamua kuwachukua watoto na kutoroka nao, tendo analoeleza hisia kwa kauli:

"Ulikuwa uamuzi mgumu kwangu kwa sababu kifedha kiuchumi nilikuwa na maisha mazuri. Lakini huwezi kuishi katika mazingira ya namna hiyo yenye vitisho na mapigano. Nililazimika kutoroka."

MAGEUZI KENYA
Hali ya uzazi nchini Kenya, inaelezwa kuwa na mabadiliko makubwa, wazazi wanaenda hospitali kujifungua tofauti na kwa wakunga.

"Walikuwa wanawaua," anafafanua Seline Okiki, Mwenyekiti wa chama kimoja cha Wakunga nchini Kenya, ambacho kina mzizi wake Magharibi mwa Kenya.

"Kama mtoto mwenye jinsia mbili anazaliwa, mara moja hutafsiriwa ni mkosi na ‘kichanga’ hicho hakiruhusiwi kuishi. Ilitarajiwa kuwa wakunga wa jadi wanamuua mtoto na kumfahamisha mama yake kuwa mtoto bado yuko hai."

Katika jamii ya kabila la Wajaluo nchini Kenya, inaelezwa kuna kanuni ya namna hata ‘kachanga’ kanavyouawa na wakunga wa jadi hutamka kauli eti ‘wamevunja viazi vitamu.”

Inaelezwa kuwa neno ‘viazi vitamu’ hutumika katika maana kwamba, ndivyo vinatumika kuvunja mifupa laini ya ‘kachanga.’

Mwenyekiti huyo wa kikundi cha wakunga kiitwacho ‘Ten Beloved Sisters’ hivi sasa wameacha jukumu la ukunga na sasa wanawapeleka wazazi hospitali.

Moja ya maeneo waliofunguka macho ni hatari ya kuambuikizwa maradhi ya Ukimwi. Hata hivyo inaelezwa kuwa, ukunga wa jadi bado unaendelea katika sehemu za ndani vijiji ambako ni mbali na hospitali.

WANAHARAKATI
Georgina Adhiambo, ni Mkurugenzi Mtendaji wa kikundi cha kujitolea kutoka Magharibi mwa Kenya kiitwacho ‘Voices of Women in Western Kenya’ ambayo sasa iko katika harakati kubwa za kupambana na unayanyapaa dhidi watu wenye jinsia mbili na mila zinazoambatana nazo.

“Tumewapitia wazazi waliojaribu kuwaficha watoto wao na hata kuwafungia ndani, wakiona aibu kutokana na hayo, huku wengine wakihofu wanaweza kudhuriwa.

" Tunafafanua wati wa jinsia mbili ni kina nani. Kuna kikundi chenye sura ya kidini, hivyo tunawaelezea kwamba watoto wenye jinsia m mbili ni sehemu ya uumbaji wa Mungu,” anasema

Hilo ndilo linaloungwa mkono na Zainab, anayesema kuwa watoto aliyo nao ni zao la umbaji wa Mungu.

DAKTARI BINGWA
Mtaalamu bingwa wa watoto, Dk. Joyce Mbogo, aliyebobea katika kushughulikia kasoro za kimaumbile katika sehemu za siri, anakiri jamii sasa imeanza kubadilika kuhusiana na suala hilo.

"Tuna aina mpya ya wazazi ambao wako tayari kuomba msaada," anasema mtaaluma huyo na anaongeza:“Intaneti sasa inafikia hata katika maeneo ya vijijini, hivyo pale wanapogundua kwamba kuna jambo halijakaa sawa, wana uwezo wa kulifuatilia."

Anasema namna ya kuwashugulikia watoto hao inatofuatiana. Kuna baadhi ya wazazi hawahitaji kabisa na wengi wanayahitaji matibabu.

Mtaalamu huyo wa tiba ya watoto anaeleza aina ya tiba inayohitajika kuwanusuru watoto hao ni pamoja na kuwapa dawa zinazoleta marekebisho katika homoni zao na wapo wanaowapenda kufanyiwa upasuaji.

Hata hivyo, kuna hoja zinazojengwa kuwa ni vyema watoto wakaamua wakishapevuka kimwili, ndiyo wafanye maamuzi ya jinsia anayoipenda.

Pia, kwa mzazi Zainab anajivuna kuwa na watoto hao aliyotoroka nao wakiwa na afya njema, wanakula na kulala vyema, pia wakifurahi vyema na watoto wake. 


Inaelezwa kuwa, licha ya kutokuwapo takwimu kamili la tauzo hilo, wastani uliopo nchini Kenya ni asilimia 1.7 ya jamii yote, ambayo inadaiwa kuwa wastani wa nchi nyingi duniani.Nipashe
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: