BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

VIONGOZI WA KUCHAGULIWA NDANI YA CHADEMA WAENDELEA KUMONG'ONYOKA KUMFUATA RAIS DK MAGUFULI ARUSHA


Rais John Magufuli

Arusha.
Chadema mkoani Arusha, imeendelea kupata pigo baada ya diwani wa tano wa chama hicho kujiuzulu ndani ya mwezi mmoja naye kama wenzake, akisema anamuunga mkono Rais John Magufuli.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, diwani huyo wa Muriet, Credo Kifukwe alitangaza kujiuzulu nafasi yake kutokana na kuridhishwa na utendaji wa Rais Magufuli.

Hata hivyo muda mfupi baada ya kikao hicho, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema alisema diwani huyo na wengine wanne waliojiuzulu katika Jimbo la Arumeru Mashariki linaloongozwa na Joshua Nassari wanashawishiwa kwa fedha na madaraka.

“Tuna taarifa kuna mkakati mkubwa wa kutumia fedha ambao unaendelea sio Arusha tu, ni kanda yote ya kaskazini, kununua viongozi waliochaguliwa lakini sisi kama Chadema hatuwezi kuwazuia wanaokubali kushawishiwa na kuondoka, kwani ni bora kubaki na viongozi wachache wenye moyo ya kuleta mabadiliko kuliko wengi ambao hawana dhamira ya kweli,” alisema.

Akizungumza katika kikao kifupi ofisini kwake, Kifukwe alikanusha kuwa amenunuliwa na kusema amejiuzulu kwa utashi wake baada ya kuridhishwa na utendaji mzuri wa Serikali.


“Nimejiuzulu mwenyewe na sitarajii kujiunga na chama kingine, nataka kufanya kazi zangu binafsi, kama mnavyonijua mimi ni mtu ambaye nipo mstari wa mbele kusimamia haki na ukweli na sina unafiki, nimejaribu kuangalia tangu nimechaguliwa, nimeona kazi anayofanya (Rais) ni nzuri na ni kazi ambazo hata wapinzani tulitaka kuifanya,” alisema.

Alisema anamuunga mkono Rais Magufuli kwa kazi anayofanya pamoja na wateule wake wote... “Anafanya kazi kwa weledi na inaleta maendeleo.”

Diwani huyo ameandika barua ya kujiuzulu kwa mkurugenzi wa jiji na muda mfupi baada ya kutangaza uamuzi huo jana, Kaimu Mkurugenzi wa jiji la Arusha, Mhandisi Gaston Gassana aliwaambia wanahabari kwamba ameipokea.

Madiwani wengine waliojiuzulu wote kutoka Jimbo la Arumeru Mashariki ni Anderson Sikawa (Leguruki), Emmanuel Mollel (Makiba), Greyson Isangya (Maroroni) na Josephine Mshiu (Viti Maalumu).

Akizungumzia kujiuzulu kwa diwani huyo wa tano, mwenyekiti wa madiwani wa Chadema Arusha, Isaya Doita alisema ni jambo lililowashtua na kudokeza kwamba Chadema ilifanya makosa kupitisha watu kugombea uongozi. 


“Hili suala lina sura nyingi inawezekana hatukuwa makini sana kupata madiwani wetu, pili labda kuna ofa miongoni mwetu lakini pia inawezekana kuna ushawishi unaendelea,” alisema.

Kuhusu madai ya kurubuniwa, Katibu wa CCM Wilaya ya Meru, Aloyce Hhayuma alisema taarifa hizo zinazosambaa mitandaoni kwamba madiwani hao wamehama kutokana na ushawishi ikiwamo kuahidiwa kiasi kikubwa cha fedha na madaraka serikalini, si za kweli.

Akizungumza na waandishi wa habari jana kabla ya Kifukwe kutangaza kujiuzulu, Hhayuma alisema sababu kubwa iliyochangia madiwani hao wanne, wakiwamo watatu wa kuchaguliwa na wananchi katika kata zao na moja wa viti maalumu ni kutokana na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya CCM chini ya Rais Magufuli.


“Hakuna ushawishi wowote uliofanyika iwe ni wa fedha, madaraka au kingine chochote. Madiwani waliohama kutoka Chadema na kujiunga na CCM walifanya hivyo kwa hiari yao kutokana na kazi nzuri ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi inayofanywa na Serikali chini ya jemedari wetu, Dk John Magufuli.”
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: