BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

DONALD TRUMP ALIFANYA TENDO LA NDOA NA MWIGIZAJI WA VIDEO ZA UTUPU NA KUTAKIWA KUTOFICHUA SIRI

Mwigizaji wa video za utupu Stormy Daniels, ambaye jina lake halisi ni Stephanie Clifford, amesema alitishiwa na kutakiwa kukaa kimywa kuhusu kufanya tendo la ndoa na Donald Trump mwaka 2006.

Ameambia kituo cha runinga cha CBS News kwamba mwanamume mmoja alifika kwake alipokuwa kwenye maegesho ya magari mjini Las Vegas mwaka 2011.

Mtu huyo ambaye hakumfahamu anadaiwa kumwambia "mwache Trump", kisha akamtazama binti mdogo wa mwigizaji huyo na kuongeza: "Itakuwa aibu sana iwapo jambo litamtendekea mamake."

Trump amekanusha vikali kwamba aliwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwigizaji huyo.

Mawakili wa Trump wanataka kulipwa fidia ya $20m (£14m) na mwanamke huyo, wakisema alikiuka makubaliano ya kuweka siri ambayo aliyatia saini katika ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2016.

Stormy amesema nini hasa?
Ameambia kipindi hicho cha Dakika 60, ambacho kilipeperushwa hewani Jumapili jioni, kwamba mwanamume huyo alimjia baada yake kukubali kusimulia kisa chake kwa jarida moja.

"Nilikuwa kwenye maegesho ya magari, nilikuwa naelekea kwenye kikao cha mazoezi niliwa nimembeba binti wangu mchanga," alisema.

"Mwanamume alinijia na kuniambia, 'Mwache Trump. Sahau taarifa hiyo'. Kisha, aliinama na kumtazama binti wangu na kusema, 'Ni msichana mdogo mrembo sana. Itakuwa ni aibu sana iwapo jambo litamtendekea mamake'. Na hivyo tu, akaondoka."

Rais Trump hajajibu madai hayo ya karibuni zaidi. Trump alirejea White House kutoka Florida Jumapili

Rais huyo alikuwa kituo chake cha gofu na hoteli cha Mar-a-Lago jimbo la Florida wikendi lakini alirejea White House kabla ya kipindi hicho kurushwa hewani.

Bi Trump hata hivyo alisalia Florida, msemaji mmoja wa White House alisema.

Nini kinadaiwa kutokea 2006?
Bi Clifford aliambia CBS kwamba mara pekee ambapo alifanya ngono na Trump ni wakati alipomwalika kwa chakula cha jioni kwenye chumba chake cha hoteli.

Anasema Trump alimuonesha jarida lililokuwa na picha yake kwenye jalada.

Anasema alilichukua jarida hilo na kumgonga Trump nalo makalioni kama utani.

"Aligeuka na kuteremsha suruali yake chini kidogo, unajua, alikuwa na suruali ya ndani na vitu vingine, na nilimgonga kidogo kidogo kwa utani," anasema.

Bw Clifford anasema ingawa hakuvutiwa kwa vyovyote vile na Trump, alifanya mapenzi naye wakati huo, akisema: "Sikukataa. Mimi si mwathiriwa."

Trump, anaongeza, alikuwa amedokeza kwamba kulikuwa na uwezekano angeshirikishwa kwenye kipindi chake cha runinga cha The Apprentice.

Anasema alichukulia mkutano wao kuwa sawa na "mkutano wa makubaliano ya kibiashara". Michael Cohen anadaiwa kumlipa Stormy Daniels $130,000 Oktoba 2016

Na pesa je?
Bi Clifford ameambia CBS alipokeza "fedha za kukaa kimya" kutoka kwa wakili wa kibinafsi wa Trump kwa sababu alikuwa na wasiwasi kuhusu usalama wa familia yake.

Amewahi kusema awali kwamba alilipwa $130,000 na wakili huyo Michael Cohen kusalia kimya kuhusu uhusiano wao huo kabla ya uchaguzi mkuu wa 2016.

Cohen alithibitisha Februari kwamba alimlipa mwanamke huyo lakini hakusema alimlipa kwa niaba ya nani.

Wakosoaji wa Trump wamedokeza kwamba kuna uwezekano pesa hizo zilikuwa sehemu ya mchango wa pesa haramu za kampeni.

Cohen alisema mwezi jana kwamba Trump na kampuni yake ya Trump Organization hawakuhusika katika kulipwa kwa pesa hizo.

Aidha, amekanusha kumtishia Bi Clifford, CBS News wameripoti.
Madai ya Stormy ni tofauti?

Bi Clifford ni mmoja kati ya wanawake watatu ambao wameanza kesi dhidi ya Rais Trump kuhusu madai ya uhusiano wa kimapenzi au udhalilishaji.

Wakili wake Michael Avenatti ameambia BBC kwamba kesi ya mteja wake ni tofauti na wengine kwa sababu inahusu "visa vya kutolewa vitisho na mbinu ambazo zilitumiwa kumnyamazisha mteja wangu."

"Nafikiri ni kisa cha kustaajabisha na kinafaa kuwashangaza sio tu Wamarekani bali pia watu katika mataifa yaliyostaarabika ya magharibi," amesema.

Ameongeza: "Hivi sivyo watu walio madarakani wanavyofaa kuendesha shughuli zao."
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: