BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

KOCHA MKUU RENARD APANGUA KIKOSI CHA ZAMBIA, NI BAADA YA KUTANDIKWA BAO 1-0 NA STARS JIJINI DAR ES SALAAM

wa ufupi

Mshambuliaji wa Stars, Mrisho Ngassa alifunga bao pekee kwenye mechi hiyo ya kirafiki ya kimataifa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wikiendi iliyomalizika.Kikosi cha baadhi ya wachezaji wa zambia kikishangilia.

 

KIPIGO cha bao 1-0 walichokipata mabingwa wa Afrika, Chipolopolo ya Zambia kutoka kwa Taifa Stars ya Tanzania, kimemshtua Kocha Herve Renard na sasa ameamua kuwatoa kwenye kikosi wachezaji wa kikosi hicho wanaocheza ligi ya ndani nchini humo.

Mshambuliaji wa Stars, Mrisho Ngassa alifunga bao pekee kwenye mechi hiyo ya kirafiki ya kimataifa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wikiendi iliyomalizika.

Akizungumza na gazeti la Times of Zambia muda mfupi baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kenneth Kaunda akitokea Tanzania, Renard alisema wachezaji wa ndani wanapaswa kuthibitisha ubora wao kwenye michezo ya kirafiki ili waweze kuingia kwenye kikosi cha Chipolopolo.

“Wachezaji wa ndani wanahitaji kuonyesha uwezo wao kabla ya kuitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa,” alisema Renard.

“Kila tunaposafiri na wachezaji wa ndani tunapata matatizo, hiyo ni ishara kwamba wanatakiwa kufanya kazi ya ziada, lakini wengi wao wamekuwa ni mzigo kwa timu,” alisema.

Renard ambaye ametwaa tuzo ya Kocha Bora Afrika wa mwaka 2012, alisema wachezaji kama Mukuka Mulenga na Saulani Phiri pamoja na kipa Joshua Titima walionyesha kiwango kizuri.

Hiyo ndiyo sababu tosha ya kuwaita kwenye kikosi chake cha wachezaji 23, atakachokitangaza siku 10 kabla ya kuanza kwa michuano ya Afrika.

Renard alisema Wazambia hawapaswi kuwa na hofu kwa matokeo dhidi ya Tanzania kwa sababu ni sehemu ya maandalizi yao, pia mechi hiyo aliwakosa wachezaji wake 12 atakaokwenda nao Afrika Kusini.

Pia, kocha huyo alionyesha shaka na viwango vya wachezaji wake, lakini ameahidi kulifanyia kazi suala hilo katika kipindi cha wiki tatu zilizobaki kabla ya fainali hizo, ambapo Zambia ipo Kundi C pamoja na Ethiopia, Burkina Faso na Nigeria.

Nahodha wa Chipolopolo, Chris Katongo, Isaac Chansa, na James Chamanga (wanacheza China) pamoja na nyota wa TP Mazembe, Rainford Kalaba, Nathan Sinkala, Hichani Himoonde na Stopila Sunzu walicheza mechi ya Tanzania.

Wakati huohuo, Stars itaingia kambini Januari 6 kujiandaa na mechi za kufuzu kucheza fainali za mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani mwaka 2014.

Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura alisema jana Stars ilivunja kambi mara baada ya mechi na sasa wanajipanga ili timu iende kuweka kambi Afrika Kusini.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: