BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

NAPOTAFAKARI YA JULIUS MAGODI, WANANCHI SASA WAMEAMKA, VIONGOZI WAKAE SAWA.

Kwa ufupi
MWAKA 2009 Serikali ya China iliwanyonga watu wawili waliotiwa hatiani katika kashfa ya maziwa ya unga yaliyosababisha vifo vya watoto sita.
 
MWAKA 2009 Serikali ya China iliwanyonga watu wawili waliotiwa hatiani katika kashfa ya maziwa ya unga yaliyosababisha vifo vya watoto sita.

Watoto wengine zaidi ya 300,000 waliugua baada ya kutumia maziwa hayo ya unga yaliyokuwa yamechanganywa na kemikali inayotumiwa kutengeneza mbolea na bidhaa za plastiki.

Zhang Yujun na Geng Jinping ndio watu pekee walionyongwa kuhusiana na kashfa hiyo. Washtakiwa wengine kumi na tisa walihukumiwa vifungo mbalimbali jela.

Zhang Yujun alikabiliwa na shtaka la kuhatarisha afya ya umma kwa kutumia njia hatari, baada ya kuuza zaidi ya tani 770 za maziwa hayo ya unga, kuanzia Julai mwaka 2007 hadi Agosti mwaka 2008.

Geng Jinping, aliyekuwa akisimamia uzalishaji wa maziwa hayo, alitiwa hatiani kwa kusambaza maziwa hayo kwa Kampuni ya Sanlu Group, ambayo sasa imefilisika, pamoja na kampuni nyingine za maziwa.

Kama hiyo haitoshi, mwaka huu mahakama nchini Afrika Kusini, iliwahukumu kwenda jela mkuu wa zamani wa polisi na mkuu wa Idara ya Polisi wa Kimataifa (Interpol) wa nchi hiyo, baada ya kutiwa hatiani kutokana na kupokea rushwa.

Matukio hayo yananikumbusha kauli ya hivi karibuni aliyoitoa Kamishna wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Profesa Paramaganda Kabudi, ambaye alisema kuwa wananchi wengi wanachukizwa na utendaji mbovu wa baadhi ya viongozi, kiasi kwamba wanapendekeza adhabu ya kupigwa risasi kwa wale watakaopatikana na hatia ya kwenda kinyume na maadili ya uongozi.

Profesa Kabudi, ambaye alikuwa akizungumzia tathmini ya maoni ya watu kuhusu Katiba Mpya, alisema kuwa suala hilo ni miongoni mwa maoni ya wananchi, yaliyojitokeza kwa kiasi kikubwa katika mchakato wa kukusanya maoni ya Katiba Mpya, unaoendelea sehemu mbalimbali nchini.

Alisema kuwa watu hawafurahii kabisa viongozi wanaoenda kinyume na maadili ya viongozi na wengine wamependekeza wanyongwe ama wapigwe risasi hadharani, hali inayoonyesha kuwa wana ghadhabu na wamechoka.

Kwa hakika, mapendekezo haya ya wananchi kuhusu viongozi wasio waadilifu yanatuonyesha kwamba, sasa wananchi hawana uvumilivu tena kuona watu waliopewa madaraka kuongoza nchi, wakijinufaisha wao, huku umma ukibaki maskini.

Mambo yanayofanyika sasa nchini, viongozi kula bila kunawa kwa kujinufaisha wenyewe raslimali za taifa, yanasikitisha na naamini ndiyo yanayowatia uchungu Watanzania hata kuona kwamba, bila ya kuwapo adhabu kali ya kunyongwa, utajiri wao utaendelea kuwanufaisha wachache.

Naamini, hakuna kitu ambacho kinawaumiza kichwa wananchi kama kuwapo kwa taarifa kwamba, kuna mabilioni ya fedha yamefichwa nje ya nchi na Watanzania wakiwamo mawaziri, lakini Serikali imeshindwa kutoa tamko.

Kwa mfano taarifa za kuwapo Sh360 bilioni za Watanzania katika benki mbalimbali nchini Uswisi, halafu mpaka leo Serikali imeshindwa kutoa maelezo ya kina, namna itakavyorejesha nchini fedha hizo nchini.

Huo ni ushahidi kuwa viongozi wetu hawana utashi wa kudhibiti wizi, ama kwa sababu baadhi yao nao wananufaika na hali hiyo.

Wachina wamefikia hatua hii ya kuwa na ujasiri wa kunyonga watu wanaojihusisha na rushwa na kupora raslimali za nchi kutokana na kujua kuwa bila ya kuwa na adhabu kali, watu wataendelea kuhujumu nchi yao.

Tunaona Watanzania nao wameona kuwa sasa kuna umuhimu wa kuwa na adhabu hiyo, ambayo huenda ikawa ndiyo mwarobaini wa kumaliza tatizo hili.

Mapendekezo haya ya adhabu kali kwa viongozi wetu wanaojihusisha na kuihujumu nchi, yanatoa picha kwamba sasa kiongozi anayeona dalili za wananchi kumkataa ni afadhali kujiondoa mwenyewe, kuliko kusubiri fedheha.

Serikali iunde chombo chenye meno ambacho kitachunguza akaunti za viongozi ndani na nje ya nchi bila kutakiwa kupata kibali cha mahakama, ili kujua kama fedha wanazomiliki zinafanana na kipato chao.

Leo ni jambo la kawaida kabisa kuona Mkurugenzi wa Shirika la Umma,waziri au mke wake, anakuwa mzabuni mkuu wa wizara.
Je, hali hii siyo wizi wa mali ya umma ?.

Naamini kabisa kwamba kampuni hiyo husika hata kama itatoa huduma mbaya, hakuna mtu atakayeweza kuinyooshea kidole.

Siyo siri, wapo viongozi wengi tu, ambao wanashiriki katika biashara ya dawa za kulevya na wengine wakiingia mikataba ya Serikali wakiwa kwenye vyumba vya hoteli usiku. Kama viongozi wanafanya haya, watu wengine watakuwaje ?.

Katika hali hii ndiyo maana leo tunashuhudia dawa feki na vyakula visivyofaa kwa matumizi ya binadamu zikizagaa mitaani, wakati kuna taasisi za kudhibiti ubora wa bidhaa kutoka nje hata zile za ndani.

Hivi tujiulize, nani anayeingiza dawa hizo na kuziruhusu kuingia mitaani? Jibu ni wazi kuwa ni viongozi wetu.

0754 304336
juliusmagodi@yahoo.com
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: