BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

DK KIKWETE AHUDHUNISHWA NA TUKIO LA KUPOROMOKA KWA GHOROFA.

Rais Jakaya Kikwete
---
Na Ikulu-Dar es Salaam

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete mchana wa jana, Ijumaa, Machi 29, 2013, ametembelea jengo lililoporomoka na kusababisha vifo vya watu na majeruhi kwenye Mtaaa wa Indira Gandhi/Morogoro mjini Dar es Salaam na amesikitishwa na kuhuzunishwa na maafa yaliyotokana na kuporomoka kwa jengo hilo.

Rais Kikwete anawapa pole nyingi wafiwa, anawapa pole nyingi walioumia na wanaoendelea kupatiwa matibabu baada ya kubanwa katika kifusi, wakiwamo watoto wadogo ambao walikuwa wanacheza chini ya jengo hilo la ghorofa 16 wakati lilipoporomoka asubuhi ya jana huku likiendelea kujengwa.

Rais Kikwete amewapongeza na kuwashukuru wananchi wote walioshiriki na wanaendelea kushiriki katika zoezi la uokoaji pamoja na vyombo na taasisi za umma na Serikali zinazoshiriki katika zoezi na kazi hiyo ya uokoaji.

Amewataka waendelee na jitihada hizo ili kama kuna watu ambao bado wamebanwa kwenye kifusi waweze kuokolewa ili wapatiwe matibabu, na kama watakuwa wamepoteza maisha basi miili yao ipatikane na iweze kupewa mazishi ya heshima yanayostahili mwanadamu.

Wakati alipotembelea eneo la tukio hilo, Rais Kikwete ametoa maelekezo mahsusi kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam, Mheshimiwa Saidi Mecky Sadik pamoja na Kamanda wa Kanda Maalum ya Polisi ya Dar es Salaam, Kamanda Suleiman Kova.

Rais amewataka kuhakikisha kuwa Mjenzi wa jengo hilo ambaye ndiye anakuwa anajenga jengo hilo, Mhandisi Mshauri aliyekuwa anasimamia ujenzi wa jengo hilo, Mhandisi wa Jiji la Dar es Salaam ambaye alitoa kibali cha ujenzi na ndiye Mkaguzi wa ujenzi pamoja na mwenye Jengo wanapatikana haraka na kuwajibishwa ipasavyo.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: