BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

SERIKALI YATISHWA ZIGO LA MIGOGORO YA KIDINI NCHINI.

Kwa ufupi
“Baada ya kufa kwa Azimio la Arusha nchi ilipoteza itikadi imara ya kitaifa, kukosekana kwa itikadi hii ndiyo kumesababisha nchi kuongozwa bila kuwa na mfumo unaoeleweka. Mambo hayo ndiyo yanayosababisha migogoro…,” alisema Profesa Mpangala.
http://www.mwananchi.co.tz
 
Dk Helen-Kijo Bisimba. 
DAR ES SALAAM.
SIKU moja baada ya maaskofu wa madhehebu ya kikiristo Tanzania kutoa tamko zito kwamba serikali ya rais Jakaya Kikwete imeshindwa kuwasaidia ili waishi kwa amani na utulivu katika nchi yao, wasomo na wanaharakati nchini wamesema migogoro ya kidini imesababishwa na ukimya wa serikali.

Wamesema kwa muda mrefu wafuasi wa dini mbalimbali nchini wamekuwa wakifanya mihadhara, mikutano na hata kutumia kanda mbalimbali kukashifu dini zingine.

lakini walifumbiwa macho na kutochukuliwa hatua yoyote, sasa tabia hiyo imeota mizizi.

Juzi maaskofu hao walitoa tamko hilo katika ibada ya Ijumaa Kuu mjini Dodoma, kusema umefika wakati ambao Wakristo wamechoka na vitendo wanavyofanyiwa na baadhi ya waumini wa dini zingine.

“Tatizo ni kuwa Serikali inashindwa kuchukua hatua mapema, makanisa yanachomwa moto visiwani Zanzibar, migogoro inazidi, lakini hakuna hatua zozote ambazo Serikali inachukua katika kunusuru hali hiyo, tumechoka,” ilisema taarifa ya maaskofu.

Wakati maaskofu hao wakieleza hayo, jana Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum aliliambia Mwananchi Jumapili kwamba Serikali inatakiwa kuwakutanisha masheikh na maaskofu ili kumaliza tofauti zilizopo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Helen-Kijo Bisimba alisema Serikali ilitakiwa kuchukua hatua miaka mingi iliyopita kwa kuwa mgogoro huu haukuanza leo.

“Migogoro ya kidini ilianza siku nyingi lakini Serikali ilikuwa kimya, wapo watu waliokamatwa kwa tuhuma za kukashifu dini za wenzao lakini hawajachukuliwa hatua yoyote,” alisema Bisimba.

Akizungumzia hali hiyo Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Profesa Gaudence Mpangala alisema migogoro hiyo ilianza kuchipua miaka michache baada ya kufa kwa Azimio la Arusha.

“Baada ya kufa kwa Azimio la Arusha nchi ilipoteza itikadi imara ya kitaifa, kukosekana kwa itikadi hii ndiyo kumesababisha nchi kuongozwa bila kuwa na mfumo unaoeleweka. Mambo hayo ndiyo yanayosababisha migogoro…,” alisema Profesa Mpangala.

Alisema jambo jingine ni kufa kwa Siasa za Ujamaa na Kujitegemea, ongezeko la umaskini na watu kukosa ajira, hivyo kuwa wepesi kushawishika kujiingiza katika migogoro ya kidini.

“Nadhani umefikia wakati wa Serikali kufuata sheria ili kumaliza hali hii, ikiwa ni pamoja na kukutana na pande zenye migogoro,” alisema Mpangala.

Mhadhiri mwingine wa Chuo hicho, Dk Kitila Mkumbo alisema Serikali inatakiwa kufanya mambo mawili ili kumaliza tatizo hilo. Jambo la kwanza ni kuzikutanisha pande zote mbili huku yenyewe ikiwa katikati na kutoegemea upande wowote.


Katika maelezo yake, Sheikh Mussa alisema, “Serikali ndiyo mlinzi wa amani hivyo inatakiwa kuhakikisha inawakutanisha watu wa pande zinazosigana kiitikadi, lakini Watanzania pia tunatakiwa kutambua thamani ya amani yetu hivyo tunatakiwa kuisaidia Serikali katika jambo hili.”

Katika tamko la maaskofu hao lililosomwa na Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Dodoma, Amon Kinyunyu alisema, “Serikali imeshindwa kuchukua hatua kwa muda mwafaka, pindi inapotokea migogoro au dini moja kutishiwa amani.”

“Matokeo yanayotokea Zanzibar mathalan, Wakristo wanaoishi huko yamewasababishia hofu, hivyo wengi kuanza kuvikimbia visiwa hivyo na kukimbiliaTanzania Bara.”

Kwa mujibu wa Askofu Kinyunyu, suala la uchomaji wa makanisa hadi sasa limeshindwa kupatiwa ufumbuzi na kila kukicha bado makanisa yanaendelea kuchomwa moto akahoji Serikali kukaa kimya maana yake nini ?.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: