BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

KIBANDA AITOA JASHO POLISI

 UPELELEZI WA SAKATA LAKE WATIA HOFU.
http://www.freemedia.co.tz
JUHUDI za Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kuwanasa watuhumiwa waliomtesa na kumuumiza vibaya Mwenyekiti wa Jukwa la Wahariri Nchini (TEF), Absalom Kibanda, huenda zikagonga mwamba kutokana na utata uliopo, Tanzania Daima limedokezwa.

Taarifa za ndani ya jeshi hilo zinadai kuwa suala hilo limeanza kuumiza vichwa huku baadhi ya askari wa chini wakikerwa na tabia ya wakubwa wao kusuasua kulimaliza.

Kibanda ambaye pia ni Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New habari (2006) Ltd, wachapishaji wa magazeti ya Rai, The African, Mtanzania, Bingwa na Dimba, alivamiwa Machi 3, mwaka huu, nyumbani kwake kisha kupigwa nondo kichwani, kutobolewa jicho, kunyofolewa ukucha, kung’olewa meno mawili na kukatwa kidole.

Wakati Kibanda akiendelea kupata matibabu nchini Afrika Kusini, mwenendo wa uchunguzi wa sakata lake umezua mashaka kutokana na mlolongo wa matukio yanayoibuliwa ili kujaribu kuzima mjadala huo.

Vyanzo vyetu kutoka ndani ya jeshi la polisi ambalo linaendelea kupeleleza tukio hilo, vilisema kuwa baadhi ya askari hawaridhishwi na kasi ndogo inayoonyeshwa katika kulipatia ufumbuzi badala yake jamii imekuwa ikidhani linahusika.

“Suala hili kwa sasa limekuwa gumu, tangu Kibanda atekwe hadi sasa, makachero tunaumiza vichwa, ingawa hatuwezi kusema wazi kuwa tumeshindwa kuwabaini watu hao.

“Lakini ukweli unajidhihirisha kuwa hicho kikundi kilichomtesa Kibanda kina wataalamu wa kazi hiyo na wala si majambazi au vibaka wa kawaida.

“Haya ni mateso ya watu maalumu wanaojua kutesa na hayo hufunzwa kwa watu maalumu kwenye vyuo maalumu,” kilisema chanzo hicho.

Chanzo hicho kiliongeza: “Inasikitisha kiasi fulani watu wanataka kujaribu kuanza kuhusisha suala la Kibanda na suala la watuhumiwa waliokamatwa kwa masuala mengine kabisa ya kisiasa.

“Hata sasa huyu ambaye tumemshikilia hapa, zote hizi ni siasa tu, watu wangependa mabega yao yapendeze, hali kama hii ikiendelea kukua ndani ya jeshi itasababisha tudharaulike.”

Baadhi ya vyombo vya habari navyo vinadaiwa kutumiwa kulififisha suala la Kibanda kwa kuibua mijadala ya kushambuliana vyenyewe kwa vyenyewe hatua inayoonekana kuwepo kwa ajenda ya siri ndani yake.

“Ni kama vile haiwezekani, kusema kuwa tangu Kibanda ateswe eti hakuna hata mtuhumiwa mmoja aliyetiwa mbaroni, hata na viongozi wetu wa jeshi la polisi ukiwauliza, wanaanza kusema timu iliyoundwa kupeleleza suala la Lwakatare (Wilfred) na Ludovick (Joseph) litashughulikia pia suala la Kibanda.

“Haya mambo mawili ya Kibanda na Dk. Stephen Ulimboka kweli yanatufedhehesha sana, tunaonekana tunafanya siasa badala ya taaluma ya ukachero, hapa kuna baadhi ya wakubwa wanalindwa; sisi tunapelekeshwa tu,” kilisisitiza chanzo chetu.

Zikiwa zimetimia siku 26 tangu kuteswa kwa Kibanda, tume ya polisi ya wataalamu iliyoundwa na Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es salaam, Suleiman Kova, haijamkamata mtuhumiwa hata mmoja huku kamanda huyo akikataa kuzungumzia maendeleo ya uchunguzi.

Tukio la Kibanda limekuwa likifananishwa na lile la Dk. Ulimboka kutokana na utaaalamu uliotumika kuwatesa kufafana ingawa yalitendeka maeneo tofauti.

Dk. Ulimboka ambaye alitekwa na watu wasiojulikana usiku wa Juni 26, mwaka jana, hadi leo ni mtu mmoja amefunguliwa mashtaka baada ya kujisalimisha kanisani akidai kuhusika na tukio hilo.

Mshtakiwa huyo, Joshua Mulundi, awali ilidaiwa na uongozi wa kanisa alikojisalimisha kuwa alikuwa na matatizo ya akili lakini jeshi la polisi limekuwa likisema upelezi wa tukio zima pamoja na uchunguzi wa afya yake unaendelea.

Dk. Ulimboka mwenyewe alimtaja mara kadhaa, mtu aliyedai ni Afisa Usalama wa Ikulu, Ramadhan Ighondu, kuwa alihusika kumteka na kumtesa, ingawa hadi leo hajawahi kuhojiwa na polisi kuthibitisha hilo.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: