BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

SIRI YA MVUTANO KATI YA SERIKALI NA BUNGE KUANIKWA LEO BUNGENI DODOMA.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge anayetarajiwa kusoma maoni ya kamati yake leo Bungeni.

Dodoma. 
Siri ya mvutano uliodumu kwa takriban wiki mbili baina ya Serikali na Kamati ya Bajeti, utawekwa hadharani leo wakati Bunge litakapoanza kujadili Bajeti Kuu.
Mjadala huo utaanza kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge kusoma maoni ya kamati yake na kufuatiwa na Waziri Kivuli wa Fedha, James Mbatia ambaye atasoma maoni ya Kambi ya Upinzani kuhusu bajeti hiyo.
Mbatia pia ni mjumbe katika kamati inayoongozwa na Chenge, hivyo hoja zao huenda zitashabihiana katika baadhi ya maoni na mapendekezo, kubwa ikiwa ni hoja ya kutozingatiwa kwa baadhi ya ushauri kuhusu vyanzo vipya vya mapato.
Kadhalika, hoja kuhusu mzigo wa madeni unaoikabili Serikali, kutokuwapo kwa miradi ya vipaumbele, kutotengwa kwa fedha za kutosha kwa ajili ya miradi ya maendeleo na kuyumba kwa bajeti inayoishia Juni 30 mwaka huu, zinatarajiwa kutawala mjadala huo.
Kuanza kwa mjadala huo ndani ya Bunge ni mwendelezo wa kile kilichokuwa kikijadiliwa kwa takriban kwa wiki mbili baina ya Serikali na Kamati ya Bajeti.
Awali kulitokea mabishano makali kutokana na kutotengwa katika bajeti fedha za kulipa madeni ya makandarasi wa ujenzi wa barabara ambayo hivi sasa yanafikia Sh800 bilioni, pamoja na kutokuwapo kwa makadirio ya fedha za kugharimia mafuta ya kuendeshea mitambo ya kufua umeme.
“Tumewauliza kwamba hizo fedha zitatoka wapi, kwa kuwa katika mafungu ya wizara hizo (Ujenzi na Nishati na Madini) hazikutengwa na hata kwenye bajeti kuu hazipo, sasa zitalipwaje, lakini hawatujibu,” kilisema chanzo chetu kutoka ndani ya kikao hicho na kuongeza:
“Tumekuwa na wasiwasi kwamba huenda fedha wanachukua kwenye makusanyo ya kodi na kusababisha kushindwa kutekeleza mahitaji mengine kwenye bajeti. Ndiyo hivyo si mnaona fedha hazikutoka kabisa mwaka huu wa fedha?”
Taarifa Hazina iliyotolewa mbele ya Kamati ya Bajeti inaonyesha kuwa kati ya Oktoba mwaka jana na Machi mwaka huu, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), lilipewa Sh578 bilioni kwa ajili ya ununuzi wa mafuta, ikiwa ni wastani wa Sh96.33 bilioni kwa mwezi.
Akisoma bajeti ya Serikali ya 2014/15, Alhamisi iliyopita, Waziri wa Fedha, Saada Nkuya Salum alitaja gharama kubwa za uendeshaji wa mitambo ya kufua umeme wa dharura na madeni makubwa ya makandarasi, wazabuni na watumishi kuwa ni baadhi ya changamoto katika utekelezaji wa bajeti ya Serikali.
Hata hivyo, alisema: “Kuhusu madai ya makandarasi na wazabuni, Serikali inakamilisha utaratibu wa kuyasimamia na kulipa madai yaliyohakikiwa kupitia Hazina kwa kushirikiana na wizara na taasisi zinazohusika.”
Suala lingine ambalo lilionekana kuitisha Kamati ya Bajeti ni ukuaji wa kasi wa deni la taifa ambalo limefikia Sh30.563 trilioni, ambalo kwa mtizamo wa wajumbe wengi ni sawa na asilimia 57.7 ya pato la taifa.MWANANCHI
 
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: