BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

ALIYEKUWA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR, BAADA YA KUNG'OLEWA MADARAKA AELEZA IPO SIKU UKWELI UTAANIKWA HADHARANI.


Aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Othman Masoud Othman

Dar es Salaam. Kung’olewa kwa aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Othman Masoud Othman katika nafasi hiyo ni kama kumewasha moto visiwani humo huku mwenyewe akisema: ‘Ipo siku ukweli utadhihirika.’


Othman licha ya kutafutwa kutwa nzima ya jana, hakuwa tayari kuzungumzia kufukuzwa kwake kazi na badala yake alituma ujumbe mfupi kupitia simu yake ya kiganjani akisema: “Si wakati wake kulizungumza.”


Alipoulizwa kwamba pengine anaweza kuwa tayari lini kuzungumzia suala hilo, Mwanasheria huyo aliyepinga baadhi ya Ibara za Katiba zinazopendekezwa kwa kuzipigia kura za hapana, alijibu pia kwa kifupi: “I have no idea when (sifahamu ni lini), time will tell (ipo siku ukweli utadhihiri)”.


Kwa upande mwingine, watu wa kada mbalimbali nchini wameelezea uamuzi wa Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein kumtimua kazi kuwa ni uonevu kwa kuwa alitumia haki yake ya kikatiba.


Mwalimu wa Idara ya Lugha za Kigeni na Isimu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Faraja Christoms alisema, “Sidhani kama ni matumizi mazuri ya madaraka. Othman katika maelezo yake alitamka wazi kuwa maoni yake si msimamo wa Serikali ya Zanzibar. Alichokizungumza ndiyo msimamo wake binafsi na jinsi anavyoona inafaa.”


Alisema Mwanasheria huyo katika maoni yake alieleza wazi jinsi Katiba ya Zanzibar inavyokinzana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano... “Kilichomtokea ni tatizo la kutokuwapo kwa maridhiano tangu ulipoanza mchakato wa kuandika Katiba Mpya.”


Mkurugenzi Mtendaji wa shirika lisilokuwa la kiserikali linalojihusisha na masuala ya kijamii (Fordia), Buberwa Kaiza alisema wajumbe wa Bunge la Katiba walipiga kura kwa utashi wao na si ushawishi kutoka katika makundi wanayotoka.


“Alichokizungumza Othman si maoni ya Serikali za Zanzibar. Alipokuwa bungeni alikuwa sawa na wajumbe wengine na si mwakilishi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Hii ni ishara mbaya kwa watendaji wa Serikali. Maana yake ni kwamba watendaji wa chini wakifichua uovu unaofanywa na walio juu yao wanaweza kufukuzwa kazi.”


Mtaalamu wa Lugha ya Kiswahili, Dk Aldin Mutembei alisema: “Sasa watu wameanza kuzuiwa kuamua mambo yao wao wenyewe. Othman alipiga kura kama yeye binafsi na si Serikali ya Zanzibar tena akiwa na mawazo huru kabisa. Kumfukuza kazi ni kutomtendea haki.”


Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema: “Ubatili siku zote huzaa ubatili. Nchi yetu sijui inakwenda wapi, maana watu wanazuiwa kufanya mambo yao ambayo yapo kikatiba. Maandamano hakuna, ukisema ukweli unafukuzwa kazi?


“Watanzania wataendelea kudai Katiba yenye maoni yao. Hii ni ishara ya kutaka kuwafumba midomo wengine wanaopenda kueleza ukweli.


Mhadhiri wa UDSM, Dk Benson Bana alikuwa tofauti na wenzake, akisema kilichomkuta mwanasheria huyo alikitarajia kwa sababu kitendo chake cha kupiga kura ya hapana kilimaanisha kuwa amekwenda tofauti na msimamo wa Serikali ya Zanzibar.


“AG anahudhuria vikao vya Baraza la Mawaziri la Zanzibar na ni lazima kuna mambo ambayo wanakubaliana, ambayo unatakiwa uyapinge ukiwa nao na si nje ya vikao vyenu.


“Alipokuwa bungeni alikuwa amebeba msimamo wa Zanzibar na kitendo cha kupiga ‘hapana’ ni kinyume na miiko ya uwajibikaji wa pamoja,” alisema Dk Bana.


Waziri wa Katiba na Sheria wa Zanzibar, Abubakar Khamis Abubakar (CUF), alisema hafahamu sababu za kigogo huyo kuvuliwa wadhifa wake.


“Aliyemwondoa AG ni Rais wa Zanzibar, yeye ndiye atakuwa anajua sababu za kufuta uteuzi wake,” alisema Abubakar.


Hata hivyo, Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS), Awadh Ali Said alisema haikuwa wakati mwafaka kwa Rais Shein kumvua wadhifa Othman wakati Taifa bado halijakamilisha mchakato wa kupata Katiba ya Muungano na Zanzibar.


Alisema alikuwa akitetea mambo hayo kwa kuweka mbele manufaa ya Zanzibar na wananchi wake pamoja na vizazi vijavyo hasa kwa kuzingatia kuwa SMZ haikuwa na msimamo wa pamoja katika suala la mabadiliko ya Katiba ya Muungano tangu mwanzo.


Alisema uamuzi wa kumvua wadhifa una madhara makubwa ikiwamo kuwajengea misingi ya woga watendaji wakuu na kujikuta wakishindwa kujitokeza kutetea au kupigania mambo ya msingi yenye manufaa kwa Zanzibar na wananchi wake.


Mwanasheria Mkuu wa zamani, Hamid Mbwezeleni alisema kwamba Rais hajafanya kosa kwa kumwondoa kwa sababu anatekeleza wajibu wake kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi kama vile alivyomchagua na Katiba inampa haki ya kumwondoa.


Naibu Katibu Mkuu wa CUF na Waziri wa Biashara Viwanda na Masoko Zanzibar, Ahmed Nassor Mazrui, alisema haikuwa busara kufukuzwa kazi wakati huu nchi ikiwa katika mjadala mkubwa wa kutafuta Katiba Mpya.


Alisema AG hakufanya makosa kutetea msimamo unaokwenda kinyume na ule wa CCM katika kutafuta Katiba Mpya kwa kuwa alikuwa akitoa maoni yake kama wajumbe wengine wa Bunge la Katiba.


Katibu Mwenezi wa CCM Wilaya ya Mjini Unguja, Baraka Shamte alisema Othman alitakiwa kujiuzulu wadhifa wake kabla ya kutimuliwa kazi kutokana na kitendo chake cha kutetea mfumo wa Muungano wa Serikali tatu kinyume na matakwa ya Serikali zote mbili ya Zanzibar na ile ya Muungano.


“AG ni sehemu ya Serikali, hakupaswa kujitokeza hadharani kupinga mfumo wa muungano wa Serikali mbili kinyume na mtazamo wa bosi wake anayetetea serikali mbili katika mfumo wa Muungano,” alisema Shamte.MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: