BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

TUME YAFICHUA UONEVU UNAOFANYWA NA JESHI LA POLISI LA TANZANIA.

 
Picha ya maktaba akionekana Prof Lipumba chini ya ulinzi wa askari wa jeshi la polisi Tanzania.

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), imesema Jeshi la Polisi lilitumia nguvu kupita kiasi pamoja na kufanya vitendo vya udhalilishaji wakati wa kumkamata Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba na wafuasi 32 wa chama hicho.


Prof. Lipumba na wafuasi hao walikamatwa na Jeshi la Polisi Januari 27, mwaka huu wakati wa vurugu za kuzuia wanachama wa CUF waliotaka kufanya maandamano kuelekea eneo la Zakhem, Mbagala, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya kumbukumbu ya miaka 14 ya mauaji ya wenzao waliouawa Januari 27, 2001 na Jeshi la Polisi Zanzibar.

Mwenyekiti wa tume hiyo, Bahame Nyanduga, alikuwa akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam kutoa taarifa ya uchunguzi wa tuhuma dhidi ya Jeshi la Polisi za kuwapiga na kuwadhalilisha viongozi na wafuasi wa CUF ambao ulianza Februari 3 na kukamilika Mei 15, mwaka huu.

Nyanduga alisema uchunguzi wa tukio hilo uliofanywa na tume hiyo ulibaini kuwa Jeshi la Polisi lilitumia nguvu kupita kiasi na kutumia mabomu ya machozi hata pale ambapo haikuhitajika kufanya hivyo na kusababisha majeraha kwa viongozi na wafuasi wa CUF.

Alisema jeshi hilo pia lilikiuka misingi ya utawala bora kutokana na maofisa na askari kushindwa kuheshimu haki za binadamu na kutozingatia matakwa ya sheria zinazoongoza jeshi hilo, kufanya udhalilishaji kwa wanachama wawili wa CUF ambao ni wanawake wakati wa kuwakamata na kuwapeleka mahabusu ya gereza la Segerea.

MAPENDEKEZO
Nyanduga alisema kutokana na hali hiyo, tume imetoa mapendekezo ambayo ni kulitaka Jeshi la Polisi liwe kuzingatia kanuni, sheria, haki za binadamu na misingi ya utawala bora katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku na pia kutolewe mafunzo kwa maofisa na askari wanaoratibu na kushughulikia masuala ya maandamano, mikutano ya raia na shughuli za vyama vya siasa.

Alisema mapendekezo mengine ni kuwa maofisa na askari wa jeshi hilo wapatiwe mafunzo ya mara kwa mara yahusuyo haki za binadamu na misingi ya utawala bora na wazingatie uhuru wa vyombo vya habari.

Nyanduga alisema kwa upande wa Jeshi la Magereza imependekeza lizuiwe mara moja kufanya upekuzi wa watuhumiwa na kuepuka udhalilishaji kwa heshima na utu wa binadamu kwani ni kinyume cha kifungu cha 12(2) na 13(6) cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema kwa upande wa CUF, kimetakiwa kitafute namna ya kuboresha mahusiano na Jeshi la Polisi ili kuondoa mivutano isiyo na tija katika shughuli za kisiasa na kizingatie sheria za nchi na ibara ya 147 (1) ya Katiba inayozuia chama chochote cha siasa kuwa na kikundi chenye mtazamo wa kijeshi.

KAULI YA CHIKAWE
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe, akizungumza na NIPASHE kuhusu mapendekezo ya tume, alisema kimsingi, Jeshi la Polisi limepewa jukumu la kulinda usalama wa nchi na raia wake na kwamba litazingatia haki za binadamu katika utekelezaji wa majukumu yake.

“Sisi hatutaki baadaye tuje tuanze kulaumiwa mambo yakiwa mabaya, ndiyo maana tunasema usalama kwanza mambo mengine baadaye,” alisema Chikawe.

Jeshi la Polisi Januari 27, mwaka huu lilitumia nguvu kuwatawanya wafuasi wa CUF kwa kurusha mabomu, risasi za moto na maji ya kuwasha na kumkamata Mwenyekiti wa chama hicho, Prof. Ibrahim Lipumba na wafuasi wengine 32.

Nguvu hiyo ya polisi ilitumika wakati wa kuzuia msafara wa mwenyekiti huyo wa CUF kuelekea eneo la Zakhem, Mbagala kulikokuwa kumeandaliwa mkutano wa hadhara uliokuwa na lengo la kutoa taarifa kwa wafuasi waliokuwa wamekusanyika kwa kuwa mkutano na maandamano yamezuiliwa na polisi.

Mkutano huo ambao ulikuwa utanguliwe na maadamano kutoka ofisi za wilaya ya Temeke kwenda Zakhem kwa ajili ya kumbukumbu ya miaka 14 ya mauaji ya wafuasi wake zaidi ya 30 waliouawa Januari 27, 2001 na Jeshi la Polisi Zanzibar wakati wa maandamano ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa Rais wa Zanzibar wa mwaka 2000.

Kutokana na purukushani hizo ilidaiwa kuwa polisi wenye silaha na virungu walitembeza kichapo kikali kwa wafuasi waliokaidi amri ya polisi kuwataka watawanyike, huku wakiwashusha waliokuwa kwenye magari.


Hata hivyo, prof. Lipumba na wenzake wanakabiliwa na kesi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kuhusiana na tukio la Mbagala. CHANZO: NIPASHE
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: