SIASA GRACE TENDEGA KUTOA JASHO NA MGIMWA JIMBO LA KALENGA MKOANI IRINGA.


Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye akimtambulisha mgombea wa Ubunge kwa tiketi ya chama hicho katika uchaguzi mdogo jimbo la Kalenga, Iringa, Godfrey William Mgimwa hivi karibuni, Mgimwa alimepitishwa rasmi kugombea kiti hicho.
Akitangaza uamuzi huo uliofikiwa katika Mkutano wa Kamati Kuu ya chama hicho, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alimtaja mgombea huyo kuwa ni Grace Tendega.
Mbowe alisema kuwa, awali vyombo vya habari vilikuwa vimemtangaza Lucas Mwenda kuwa ndiye atakayewania nafasi hiyo, jina ambalo halikuwa limepewa baraka na Kamati Kuu yenye uamuzi wa mwisho.
Akifafanua zaidi, Mbowe alisema kuwa ingawa Lucas Mwenda alipata kura 132, Kamati Kuu imempitisha Grace Tendega aliyepata kura 122.
Akizungumzia sifa za Mwenda, Mbowe alisema: “Bwana Sinkala (Mwenda) bado kijana mdogo, mwanasheria wetu na tunahitaji kumkuza zaidi, basi vyombo vyote vimeshauri nafasi hii apewe mama Tendega kwa sababu ana sifa za kutosha,” alisema Mbowe.
Alifafanua kuwa uchaguzi uliofanyika Iringa ulikuwa ni sehemu tu ya vigezo vinavyotumiwa na chama kumpata mgombea mwenye sifa na ushawishi kwa wanachama wake.
“Chama chetu kina utaratibu tofauti na vyama vingine, tunampata mgombea kwa vigezo vingi na siyo kimoja, hususani vigezo vinne vinavyovingatiwa,” alisema Mbowe.
Alivitaja vigezo hivyo kuwa ni pamoja na Kamati ya Utendaji kutoa mapendekezo, kusikiliza maoni ya wadau na viongozi mbalimbali, maoni ya viongozi wa chama katika jimbo na maoni ya kiutafiti dhidi ya wagombea kwa njia ya kiintelijensia.
Pia, Kamati Kuu ya Chadema iliwapa nafasi wagombea wote 14 wanaowania nafasi hiyo kupigiana kura ya kumchagua mtu wanayedhani anafaa kupitishwa na chama kupeperusha bendera ya nafasi ya ubunge.
“Tunafanya hivyo kwa sababu tunataka mshikamano mkubwa ndani ya chama kabla na baada ya uchaguzi,” alisema Mbowe.
Mwenyekiti huyo alisema kuwa kwa mara ya kwanza Chadema itamsimamisha mgombea mwanamke katika uchaguzi mdogo wa ubunge.
“Amepitishwa na Kamati Kuu kwa kura zote, bila hata mmoja kukataa…ni kutokana na ushauri mpana uliotolewa,” aliongeza.

0 comments:
Post a Comment