BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

SIMBA SC ILIVYOPENYA TUNDU LA SINDANO MBELE YA MBEYA CITY LIGI KUU YA VODACOM TANZANIA BARA UWANJA WA SOKOINE JIJINI MBEYA.


Mshambuliaji wa Simba, Haruna Chanongo (jezi nyekundu) akizuiwa na wachezaji wa Mbeya City, Peter Mapunda (kushoto) na Paul Nonga (wapili kushoto), katika mchezo wa Ligi Kuu kwenye Uwanja wa Sokoine Mbeya. Timu hizo zilitoka sare 1-1. Picha na Michael Matemanga.  

MBEYA. 
MBEYA City wamepoteza nafasi ya kukalia usukani wa Ligi Kuu baada ya kulazimishwa sare 1-1 na Simba jana kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya.


Mbeya City walikuwa wa kwanza kupata bao lililofungwa kwa mkwaju wa penalti na nahodha Deogratius Julius, kabla ya Mrundi, Amis Tambwe kuisawazishia Simba dakika ya 50, likiwa ni bao lake 15 msimu huu katika Ligi Kuu.

Kwa matokeo hayo, Mbeya City imefikish pointi 35, sawa na Yanga (35), Simba imebaki nafasi ya nne wakiwa na pointi 32, huku Azam wakiendelea kuongoza kwa pointi 36.

Kocha wa Simba, Zdavko Logarusic alimwanzisha kipa Yaw Berko badala ya Ivo Mapunda pamoja na viungo Henry Joseph na William Lucias wakicheza katika nafasi za beki wa pembeni.
Simba walianza mchezo huo kwa kasi ambapo katika dakika ya  6, Ramadhani Singano alikosa bao akishindwa kumalizia krosi ya Haruna Chanongo.


Wenyeji Mbeya City walipata penalti dakika ya 12 baada ya beki Joseph Owino kushika mpira uliopigwa na Deus Kaseke na mwamuzi Mathew Akrama.

Nahodha wa City, Julius aliwainua mashabiki wao kwa kufunga mkwaju huo wa penalti kwa kumwacha kipa Berko asijue la kufanya.

Baada ya bao hilo Simba walirudi uwanjani na kutawala sehemu kubwa ya mchezo huo, lakini mashuti ya Singano, Tambwe na Chanongo yaliokolewa na kipa wa City, David Burhan.

Benchi la ufundi la Simba, likiongozwa na Kocha wa Logarusic, Seleman Matola, Idd Pazi na Nico Nyagawa walimvamia mwamuzi Akrana baada ya mapumziko wakipinga penalti aliyowapa City.

Simba walisawazisha bao hilo dakika ya 50, kupitia Tambwe aliyepokea pasi nzuri ya Chanongo ndani ya eneo la hatari na kupiga shuti la juu na kumwacha kipa David Burhani asijue la kufanya.

Awali mashabiki wengi waliruka ukuta kuingia uwanjani katika jukwaa lililokaliwa na mashabiki wa Mbeya City.

Pia, wachezaji wa Simba walizuiwa kuingia uwanjani kwa muda kutokana na vurugu za mashabiki zilizotokea kwenye mlango wa kuingia uwanjani hadi polisi walipoingilia kati na kutuliza hali hiyo. MWANANCHI.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: