BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

Ndoa zilizodumu muda mfupi nchini Tanzania


Dar es Salaam. Wakala wa Usajili, Udhamini na Ufilisi (Rita) imesema licha ya ndoa kuwa muungano wa hiari unaokusudiwa kudumu muda wote wa maisha ya wahusika, kuna wanandoa ambao hawajatimiza hata mwaka mmoja wa ndoa.

Miongoni mwa ndoa zilizorekodiwa na wakala huo kudumu kwa muda mfupi, ni ile iliyovunjika baada ya miezi minane na siku mbili.

Takwimu kutoka Rita, zinaonyesha kuwa ndoa hiyo ilifungwa Januari 8, 2010 na hati ya talaka ilitolewa Septemba 10, 2010.

Ndoa inayofuatia ilidumu kwa miezi tisa na siku 20 wakati nyingine ilidumu kwa mwaka mmoja na miezi mitatu.

Kwa mujibu wa Rita, huenda ndoa hizo zilidumu kwa muda mfupi zaidi kwa kuwa mchakato wa kupata talaka huwa ni mrefu.

Meneja wa Mawasiliano, Taarifa na Elimu kwa Umma wa Rita, Josephat Kimaro alisema: “Kutokana na mchakato wa talaka ulivyo, inawezekana wanandoa hao walikuwa wamechana muda, lakini kwa rekodi zetu tunaangalia siku hati ya talaka ilipotolewa.”

Ndoa nyingine iliyodumu kwa muda mfupi ni ya Annapita Salaka, mkazi wa Mwanza ambaye aliieleza Mwananchi kuwa alifunga ndoa na mume wake (jina linahifadhiwa kwa sababu hatukumpata kuzungumza naye) Juni 12, 2009, lakini ilidumu kwa wiki mbili.

“Tuliachana kienyeji kwa sababu ni vigumu ndoa ya Kikristo kuvunjwa kwa talaka, niliachana naye kwa sababu niligundua alioa na ana watoto wanne, jambo ambalo hakuniambia mapema,” alisema.

Ndoa ya muda mfupi duniani

Ndoa iliyovunja rekodi ya dunia kwa mujibu wa kitabu cha rekodi za Guinness ni kati ya Rudolph Valentino na muigizaji wa filamu, Jean Acker mwaka 1919 nchini Marekani.

Bibi harusi huyo alianza kujutia uamuzi wake wa kuolewa usiku wa kwanza baada ya kufunga ndoa.

Baada ya sherehe, inaelezwa alimfungia mume wake mlango wa chumba chao cha fungate na hapo walianza mchakato wa talaka. Ndoa nyingine inatajwa na tovuti ya Gazeti la The Standard Daily la Kenya kati ya Boniface Oduor, mkazi wa Mombasa nchini humo ambayo ilidumu kwa siku 13 baada ya Oduor kumfumania mke wake, Sarah Kayuga na mwanaume mwingine.MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: