BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

NAMUNGO FC YARUKA MITA 100 KUBEBWA KUCHEZA LIGI DARAJA LA PILI NA TFF.

Mshabuliaji wa Namungo FC ya Nachingwea mkoani Lindi, Shabaan Abdalah akimzuia mlinzi wa Mawenzi Market FC Morogoro, Hassan Ngozi wakati wa mchezo wa ligi daraja la pili uliofanyika kwenye uwanja wa jamhuri mkoani hapa ambapo mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bao 1-1.

Juma Mtanda, Morogoro.

Uongozi wa timu ya soka ya Namungo FC ya Nachingwea mkoani Lindi imekanusha vikali kubebwa na shirikisho la soka Tanzania (TFF) kucheza ligi daraja la pili 2016/2017 badala ya timu ya Stend Misuna FC ya Singida.

Akizungumza na MTANDA BLOG mbele ya mashabiki wa timu ya soka ya Mawenzi Market FC mara baada ya kumalizika kwa mchezo kati ya Namungo FC uwanja wa jamhuri Morogoro, Katibu Mkuu Mtendaji wa timu hiyo ya soka ya Namungo FC, Ally Suleiman alisema kuwa TFF haikuibeba timu yao kuingia na kucheza ligi daraja la pili.

Makumbusho FC ilikata rufaa kwa madai ya Stend Misuna FC na Namungo iliwatumia wachezaji walikosa sifa katika ligi ya mabingwa wa mikoa na Namungo ilishinda rufaa hiyo baada ya TFF kusikiliza pande zote na wao kuonekana hawana makosa.

Akitoa ufafanuzi Suleiman alisema kuwa timu ya Makumbusho FC ya Dar es Salaam ilikata rufaa kuwakatia rufaa wachezaji wanne mmoja wa timu ya Namungo FC na wachezaji watatu wa timu ya Stend Misuna FC ilionekana Namungo FC haikuvunja sheria katika kumtumia mchezaji wake ligi ya mabingwa wa mikoa kituo cha Morogoro ya kusaka timu ya kucheza ligi daraja la pili.

Suleiman alisema kuwa kwa upande wa Namungo FC mchezaji, Emmanuel Mwanga alikatiwa rufaa kwa madai ya kucheza ligi daraja la kwanza katika timu ya Kurugenzi Njombe FC iliyopo ligi daraja la kwanza Tanzania bara akitumia jina la Iman Vamwanga lakini Namungo ilimsajili mchezaji huo kutoka timu ya Timberland FC ya Lindi inayoshiriki ligi daraja la tatu ngazi ya mkoa.

“TFF haijaibeba timu ya Namungo FC wala kuipendelea kwa jambo lolote lile kuingia kucheza ligi daraja la pili, hesabu zipo wazi sana na mtu wa soka hawezi kuishutumu TFF kuwa imefanya upendeleo isipokuwa rufaa ilikuwa imekatwa ndio imetusaidia sisi kuingia ligi daraja la pili baada ya kuonekanaa hatuna hatia.”alisema Suleiman.

Stend Misuna FC ndio walioibuka vinara katika ligi ya mabingwa mikoa 2016/2017 kituo cha Morogoro kwa kukusanya pointi 13 huku Namungo FC ikiishia na pointi 12 lakini timu hizo zilidaiwa kukiuka sheria za kuwasajili wachezaji waliocheza ligi ya juu.

“Emmanuel tayari amefungiwa mwaka mmoja kucheza soka baada ya kugundulika kutumia majina mawili tofauti na TFF, Kurugenzi Njombe FC iliyopo daraja la kwanza anadaiwa alitumia jina la Iman Vamwanga wakati akicheza huko na Namungo FC sisi tunamsajili ametumia jina la Emmanue Mwanga lakini tulimsajili katika timu ya Timberland ya Lindi iliyopo ligi daraja la tatu ngazi ya mkoa.”alisema Suleiman.

Aliongeza kwa kusema kuwa uongozi wa timu yao ulipeleka vielelezo juu ya mchezaji huo katika kamati ya TFF inayoshughulikia rufaa na ilionekana wapo sahihi kumsajili mchezaji wa ligi ya chini kama sheria inavyotaka lakini wenzao wa Stend Misuna FC hawakuweza kupeleka vielelezo vya wachezaji wao watatu wanaotuhumiwa kucheza ligi ya juu katika msimu mmoja katika vikao hivyo.

“Baada ya TFF kuona timu ya Namungo FC haijatenda kosa na Stend Misuna FC kushindwa kupeleka vielelezo vya wachezaji wao watatu, walipokonywa nafasi ya kwanza na kutupa sisi ambao tulishika nafasi ya pili sasa hapo unawezaje kusema kuwa TFF imetubeba sisi ?....hapa ndipo wadau hawajaweza kuelewa.”alisema Suleiman.

Ufafanuzi huo ulitokana na madai ya shabiki wakiwarushia maneno wakati wa mchezo na baada ya kumalizika kuwa timu ya Namungo FC imetinga kwenye ligi hiyo kutokana na kubebwa na shirikisho la soka Tanzania TFF.

Mmoja wa mashabiki hao aliongea na gazeti hili ni, Shukuru Seleiman aliyedai kuwa Namungo FC imebebwa na TFF kuingia kwenye ligi ya daraja la pili badala ya Stend Misuna FC ya Singida lakini na kuwabeza kuwa kitendo cha kutoa sare na Mawenzi Market FC ya bao 1-1 inaonyesha kuwa hawana kikosi kizuri cha ushindani.

“Ninyi Namungo FC hamuwezi kufika popote kwa soka hili yaani nilijua kabisa Mawenzi Market FC atapigwa bao 4, haya ndio madhara ya kubebwa, ona sasa TFF inapata aibu, tunajua mna uchumi nzuri lakini kwanini hamkusajili wachezaji wazuri wenye hadhi ya kuchezea Namungo FC.?alihoji shabiki huyo.

Katika mchezo huo wa ligi daraja la pili kati ya Mawenzi Market FC dhidi ya Namungo ulimalizika kwa sare ya bao 1-1.

Namungo FC walipata bao la kuongoza dakika ya 43 baada ya mlinzi wa Mawenzi Market FC, Juma Senkumbo kujifunga wakati wa harakati za kuokoa mpira uliopigwa na mshambuliaji wa Namungo FC, Ahemed Chimpole na kujaa wavuni.

Mawenzi Market FC ilisawazisha bao hilo dakika ya 75 kupitia kwa mshambuliaji, Jeiran Amim baada ya kumzidi maarifa beki wa Namungo FC, Yunuj Kambi aliyeshindwa kuondosha hatari eneo la hatari baada ya kushambuliwa katika lango lao.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: