BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

MWANACHAMA WA CHADEMA ACHOMWA MKUKI MOROGORO

Juma Mtanda, Morogoro.

Mkazi wa mtaa wa Sanivina kata ya Kichangani, Martha Maeda (33) amelazwa katika wodi namba tatu hospitali ya rufaa mkoa wa Morogoro baada ya kudaiwa kujeruhiwa kwa kuchomwa mkuki katika mkono wake wa kulia majira ya saa 10 alfajili ya Januari 15 mwaka huu.

Tukio hilo linalodaiwa kuhusishwa na vuguvugu za siasa katika uchaguzi mdogo wa udiwani kata ya Kiwanja cha Ndege mkoani hapa ambapo Martha Maeda ni mwanachama wa chama cha demokrasia na maendeleo  (Chadema).


Akizungumza na mwandishi wa gazeti hili hospitali ya mkoa mjini hapa jana, Martha Maeda alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 10 alfajili baada ya kambi yao kuvamiwa na watu wenye silaha za jadi katika mtaa wa Kimunyu kata ya Kiwanja cha Ndege wakati wakiandaa chai kwa ajili ya kuondoa baridi.


“Nilichomwa mkuki majira ya saa 10 alfajili baada ya mimi na wenzangu watatu tulivyoamka ndani na kwenda nje ili kuandaa moto kwa ajili ya kuchemsha chai na muda mfupi ilipita gari ndogo na kusimama usawa wa nyumba tuliyoweka kambi na kutelemka ambapo wanaume hao wasiopungua wanne walikuwa na silaha kama mapanga, rungu, sime, fimbo, mkuki na kutuvamia.”alisema Martha.


Baada ya watu hao kuwavamia, wenzake watatu walifanikiwa kukimbia na yeye alipojaribu kukimbia alinaswa na kuni mguuni kisha kuanguka chini na mmoja wa wavamizi hao kumchoma mkuki katika mkono wake wa kulia akiwa chini na damu kuanza kutoka lakini alifanikiwa kuuchomoa na wahalifu hao waliingia kwenye gari na kutokomea eneo hilo.alisema Martha.


Mganga Msaidizi wodi namba tatu ya akinamama hopsitali ya rufaa mkoa wa Morogoro, Dk John Muneja alithibitisha kumpokea majeruhi, Martha Maeda majira ya saa 11 alfajili januari 15 mwaka huu akiwa amejeruhi katika mkono wa kulia baada ya kujeruhiwa na kitu chenye nja kali.


“Martha tulimpokea na kumpatia huduma ya kwanza na sasa anaendelea vizuri na matibabu na tutaangalia na maendeleo yake.”alisema Dk Muneja.


Msemaji wa chama cha demokrsia na maendeleo (Chadema) wilaya ya Morogoro mjini, Shabaan Dimoso alieleza kusikitishwa na tukio hilo na kudai ni mbinu chafu zinazofanywa na wapinzani wao ili kuwadhoofisha katika kampeni za uchaguzi mdogo wa kata ya Kiwanja cha Ndege ambapo wamemsimamisha mgombea.


“Hili ni tukio la nne kufanyiwa chama chetu na hii inatokana na chuki zenye lengo la kuudhoofisha upinzani hasa Chadema jambo ambalo sio sahihi kwa mustakabali wa misingi ya katiba ya nchi hii yenye kufuata misingi ya haki.”alisema Dimoso.


Dimoso alieleza kwa kudai kuwa Chadema imekuwa ikiandamwa kwa kufanyiwa matukio yasiyo ya kiungwana kutoka kwa wapinzani wao lakini na jeshi la polisi wilaya ya Morogoro mjini nalo likihusika kufanya hujuma.


“Hapa Chadema tayari tumepoteza kompyuta mpakato (Laptop) mbili ambapo moja imechukuliwa kinguvu na askari wa jeshi la polisi na nyingine ikiharibiwa vibaya kwa kuivunja jana (juzi) jioni na askari hao hao baada ya kumalizika kwa mkutano wa hadhara wa kumnadi mgombea wetu katika mtaa wa Bondwa.”alisema Dimoso.


Dimoso alidai kuwa Laptop hizo zilikuwa zikitumika kwa ajili ya kupiga nyimbo za kuhamasisha wananchi na kuendeshea vipaza sauti katika spika wakati wa mikutano ya kampeni ya kumnadi mgombea udiwani wa Chadema kata ya Kiwanja cha Ndege, Salum Milindi.


Akielezea tukio la mwanachama wao kuchomwa mkuki, Dimoso alisema kuwa hilo sio tukio la kwanza kuvamiwa katika kambi ya Chadema kwani Januari 13 majira ya saa 2 usiku mwaka huu, mtu mmoja alivamia kambi hiyo akiwa na panga kisha kudhibitiwa na baadaye taarifa ilitolewa jeshi la polisi na kupewa Mor/RB/529/2017.


Dimoso ametoa wito kwa vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi huo kuwa kufuata taratibu, sheria na kanuni za uchaguzi ili kuendeleza amani katika kipindi hiki cha kampeni na hatimaye siku ya kupiga kura.


Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Leonce Ferdinad amethibitisha kupokea taarifa za mtu mmoja kujeruhiwa na mkuki na tukio hilo linafanyiwa uchunguzi ili hatua kali za kisheria zichukuliwe.


Ferdinand alisema jeshi la polisi linachunguza tukio la mwanamke kuchomwa mkuki na kulazwa hospitali ya rufaa mkoa wa Morogoro na hawana taarifa za askari wa jeshi hilo kuchukua ama kuharibu kompyuta mpakato mbili (Laptop) na endapo taarifa itatolewa hawatasita kulifanyia uchunguzi.


“Tumepokea taarifa za mwanamke kuchomwa mkuki katika mkono majira ya saa 10 alfajili Januari 15 mwaka huu lakini tukio la Chadema kudai jeshi la polisi imeharibu kompyuta mpakato na moja kuishikilia taarifa hizo bado hajafika.”alisema Fernandi.


Ferdinand alisema kuwa matukio yote yaliyofanyika ni kinyume na sheria hivyo kama kuna mtu atapeleka malalamiko yatafanyiwa kazi kwani hakuna mtu aliye juu ya sheria haijalishi ni askari ama laa uhalifi ni uhalifu tu

Kaimu kamanda huyo aliongeza kwa  kusema kuwa jeshi la polisi ndilo lenye jukumu la kuchunguzu matukio yote ilimradi taarifa imetolewa na kutolea ufafanuzi.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: