BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

WANAWAKE 405,000 WA TANZANIA WATOA MIMBA KWA SIRI HUKU WAKIPATA MATATIZO LUKUKI KILA MWAKA


CHAMA cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA), kimebaini kuwa wanawake 405,000 nchini sawa na asilimia 40, kila mwaka hutoa mimba kwa siri na kupata matatizo huku wakishindwa kupata matibabu yanayohitajika.

Kauli hiyo ilitolewa juzi na Wakili wa Kujitegemea, Anna Shimba, wakati wa kikao cha kutokomeza vitendo vya utoaji mimba kilichoandaliwa na TAWLA jijini hapa.

Wakili Shimba alisema takwimu zinaonesha utoaji wa mimba usio salama unatajwa kama sababu ya pili ya vifo vingi vya wanawake na wasichana hapa nchini ambao baadhi yao hufanya bila kutambua kwamba ni kosa kisheria.

“Tafiti zinaonyesha kila mwaka wanawake wa Tanzania milioni moja hupata mimba zisizotarajiwa, asilimia 39 huishia kwenye utoaji wa mimba hizo, asilimia moja huzilea na kujifungua salama na asilimia 60 hupata matatizo yanayotokana na utoaji mimba lakini hawapati huduma ya matibabu wanayohitaji kwa wakati mwafaka,” alisema Shimba.

Alisema kila mwanamke mmoja kati ya watano hapa nchini ana mahitaji yasiyofikiwa na mpango wa uzazi.

Shimba alisema ili kupunguza vifo vitokanavyo na utoaji mimba usio salama na madhara yake, ipo haja vipengele vinavyohusu haki ya afya ya uzazi vilivyopo kwenye mkataba wa nyongeza ya Afrika kuingizwa kwenye sheria za hapa nchini.

Akizungumza na gazeti hili, mwezeshaji wa kikao hicho ambaye ni Mkurugenzi wa Shirika la Kutetea Haki za Wanawake Kivulini, Yassin Ally, alisema tafiti zinaonesha kuwa mwaka 2010 wasichana wa kati ya umri wa miaka 20 hadi 24 ambao ni chini ya asilimia 20 ndio hufanikiwa kuhitimu elimu ya sekondari ikilinganishwa na asilimia 32 ya wavulana.

Ally alisema wanafunzi wengi hukatisha masomo yao kutokana na kupata ujauzito na kwa mwaka 2010 wanafunzi 68,000 walikatisha masomo ya elimu ya msingi na 66,000 sekondari.

“Kwa mujibu wa takwimu hizo, Mkoa wa Mwanza ndio unaoongoza kwa kuwa na wasichana 7,000 wa shule za msingi na sekondari waliokatisha masomo yao mwaka 2010 kutokana na kupata mimba, sababu mbalimbali zinazotajwa kuchangia tatizo hilo ni umbali wa kutoka wanapoishi kwenda shuleni huku wengine wakilazimika kutembea kilomita tatu hadi 15 na njiani hukutana na vishawishi vya lifti za bodaboda kwa malipo ya ngono na kubakwa,” alisema Ally.Mtanzania
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: