BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

KESI YA FATMA KARUME DHIDI YA EUNGENE NA WARAKA WA BASHIR YAKUB

KESI YA FATMA KARUME DHIDI YA EUNGENE NA WARAKA WA BASHIR YAKUB (+255784482959).Askari yeyote anachukuliwa hatua kwa namna tatu.(1) Malalamiko ya ndani(2) Mashtaka ya jinai (3) Shauri la madai. Karume amechukua la tatu, shauri la madai.

1.MALALAMIKO YA NDANI.
Huitwa "internal Complaint". Hapa utamshitaki askari kwa wakubwa wake au mamlaka za ajira yake. Ni katika kosa lolote lile na mtu yeyote anaruhusiwa kutumia njia hii. Pia ni njia inayotumiwa na askari wenyewe kwa wenyewe wanapolalamikiana.

2. MASHTAKA YA JINAI.
Unaweza kumshtaki askari katika makosa yote ya jinai yaliyo katika Kanuni za Adhabu, Sura ya 16 , na sheria mtambuka kama ile ya rushwa, uhujumu uchumi na ya kuzuia dawa za kulevya na nyingine zote.

Mnakumbuka kesi ya iliyomhusu aliyekuwa Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP)Abdallah Zombe, Mratibu wa Polisi (SP) Christopher Bageni na wengine. Ilikuwa ya jinai na Bageni alihukumiwa kunyongwa.

3. SHAURI LA MADAI.
Askari pia hushitakiwa kwa madai. Makosa ya kila siku ya madai kwa askari ni kama, Kufunga kwa hila(false imprisonment), Kushitaki kwa hila(malicious prosecution), kudhalilisha(defamation), matumizi ya nguvu yaliyovuka mipaka(excessive force), kunyanyasa(brutality), kushika kwa hila(battery) nk.

Fatma analalamika hapa kwenye madai. Na analalamikia kushikwa/kuguswa(battery).

4. KESI YA FATMA KUSHINDWA.
i ) Nini Maana ya kushika.
Mahakama imetafsiri Kushika/kugusa(battery) katika kesi ya Mantage&Chacha Vs Mwita(1971)HCD, 110 kuwa, " Ni matumizi ya nguvu kwa mtu mwingine kinyume cha sheria".

Ili ushinde kesi yoyote ya kugusa(battery)ni LAZIMA uthibitishe kuwa kugusa huko hakukuwa halali(kinyume cha sheria).

Ndio maana mgonjwa hawezi kumshtaki daktari kwa kumgusa, au mtoto amshtaki mzazi au mwanafunzi amshtaki mwalimu,kadhalika askari anapokamata(arrest).
Ugusaji wa hawa ni halali labda waguse vinginevyo.

Eugene alimgusa Fatma, yes, ila swali ni kama ugusaji huo ulikuwa kinyume cha sheria au haukuwa halali.

Kwa Eugene ni rahisi kusema tu kuwa ugusaji ulikuwa halali kwasababu Mimi kama askari nilikuwa namzuia kufanya mkusanyiko eneo la mahakama baada ya kumwonya asifanye hivyo na kukaidi.

Video inamwonesha Fatma akiwa amefuatwa na wafuasi wengi wa Chadema eneo la mahakama huku askari wakimsihi kuondoka.Inamwonesha akikaidi mpaka alipolazimishwa kwa kuguswa mkono.

Mazingira kama haya ni rahisi kuthibitisha kuwa kuguswa kulikuwa halali na hasa ikizingatiwa aliguswa mkono na sio maeneo mengine kama makalio, matiti nk.
Kesi inaweza kufia hapa.

ii ) Pia Eugene anatakiwa kuthibitisha kuwa alitumia nguvu ya kadri alipomgusa(reasonable force). Kesi ya John Nyamhanga vs R(1980)TLR 6 inaongelea hili.

Video haioneshi Fatma akisukumwa au akivutwa. Ni alishikwa tu mkono. Hii ni nguvu ya kadri kisheria.
Hoja hii nayo inaua kesi.

Kwa ufupi ukitizama kesi hii utaona kabisa imefunguliwa kwa hasira na inakosa nguvu hasa ukizingatia kuwa aliyegusa ni askari ktk mazingira ya kutunza amani, hakugusa sehemu mbaya na hakutumia nguvu nyingi.

5. KUHUSU MAWAKILI 29.
Kuna taarifa kuwa Karume atawakilishwa na Mawakili 29.

Kushinda kesi sio utitiri wa Mawakili. Hawa hata wawe laki moja ushindi wa kesi hubaki katika mambo matatu, (1) Ukweli wa kilichotokea "facts of the case (2) Sheria inavyosema kuhusu hicho kilichotokea " legal basis" na (3) Ushahidi ulionao kuhusu hicho kilichotokea "Evidence = witness + exhibits".

Pili, Mawakili hata wawe laki moja bado anayezungumza ni mmoja. Hawawezi kuzungumza kwa mkupuo. Akizungumza mmoja mwingine lazima anyamaze. Kwa hiyo ni vilevile tu huku mmoja na kule mmoja.

Kuanzia leo mkisikia habari ya Mawakili weengi katika kesi zilizopo au zinazokuja semeni tu hizo ni mbwembwe ama SWAGA.

6. KUMSHITAKI ASKARI KAMA ASKARI.
Kama Karume amemshitaki Eugene kama Eugene na peke yake basi tutashuhudia mahakama ikiamuru kuliunganisha jeshi la polisi na mwanasheria mkuu wa Serikali.

Makosa ambayo hutendwa katika utekelezaji wa majukumu mwajiri/ofisi huunganishwa. Mnakumbuka kesi Namba 20/2017 ya mbowe na mkuu wa Wilaya ya Hai ambapo Mwanasheria mkuu wa Serikali ataunganishwa.

7. KARUME NAYE ANAKABILIWA NA KULIPA GHARAMA.

Akishinda Karume atalipwa pesa alizoomba. Lakini si lazima alipwe zote mahakama inaweza kupunguza.

Lakini naye akishindwa anakabiliwa na kulipa gharama kwa wale aliowashitaki.Kwahiyo mchezo si salama pande zote mbili.

8..VITISHO VYA KIZIMBANI .
Yapo maneno kuwa fulani sasa atakoma kwa kusimama kizimbani.

Hatuna kizimba kwenye madai. Ni kwasababu hatuna mshtakiwa(accused) bali tuna mlalamikiwa(defendant).

Pia Karume atatakiwa kujieleza na kuulizwa maswali na upande wa Eugene kama ambavyo yeye atafanya kwao. Kwahiyo kibano kiko pande zote tena kwa usawa kabisa.

Mwisho tutarajie kumuona Tundu Lissu akimwakilisha Karume kama yeye anavyomwakilisha katika jinai Kisutu.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: