BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

YANGA MIKONONI MWA MTIBWA SUGAR UWANJA WA JAMHURI MORO KATIKA MCHEZO WA LIGI KUU TANZANIA BARA LEO.

 KOCHA mkuu wa klabu ya Yanga, Mholanzi Hans van Der Pluijm akisimamia wachezaji wake katika mazoezi kwa ajili ya mchezo dhidi ya Mtibwa Sugar utaofanyika kwenye uwanja wa jamhuri mkoani Morogoro leo, Mazoezi hayo yalifanyika kwenye uwanja wa SUA mkoani hapa. PICHA ZOTE NA MTANDA BLOG.
Yanga inaingia katika mchezo huo baada ya kuibuka na ushindi mnono wa bao 2-0 mbele ya watani zao wa jadi Simba kwa mabao ya Washambuliaji Amis Tambwe na Busungu katika uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam uliofanyika hivi karibuni, Je kwa Yanga itaweza kuendeleza furaha kwa mashabiki kutokana na timu ya Mtibwa Sugar imekuwa ikipata matokeo mazuri katika michezo yake waliokutana katika ligi hiyo hivi karibuni.

Wakati Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara inatarajia kuendelea tena leo katika viwanja saba nchini,  Kocha Mkuu wa Yanga, Hans van Pluijm, amesema kikosi chake kitashuka kwenye Uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro kuikabili Mtibwa Sugar kikiwa na jukumu moja la kusaka pointi tatu muhimu.
Pluijm alisema kuwa licha ya kuwakosa nyota wake wawili wa kikosi cha kwanza ambao ni Haruna Niyonzima, ambaye amefiwa na dada yake na kulazimika kurejea Rwanda na Mbuyu Twite anayetumikia adhabu ya kadi nyekundu, hana wasiwasi na mchezo wa leo.
Akizungumza na gazeti hili jana, Pluijm, alisema kuwa haumizi kichwa kuwakosa wachezaji hao kwa sababu ana wigo mpana wa kuchagua nyota wengine wa kuziba nafasi hizo.
“Wachezaji waliopo watafanya kazi ile ile, najua mchezo utakuwa mgumu kwa sababu Mtibwa Sugar ni timu nzuri na imepata matokeo mazuri katika michezo yote, lakini nitatumia mfumo ambao utanipatia matokeo mazuri,” alisema Pluijm.Aliongeza kuwa kikosi chake hakitakuwa na mabadiliko makubwa kiuchezaji ukilinganisha na kile kilichocheza dhidi ya Simba na hiyo inatokana na kasi na ‘njaa’ ya kuhakikisha ushindi unapatikana kwenye mechi zote.
“Uchezaji wetu katika mechi ya kesho (leo) utategemea na kasi ya wapinzani wetu pamoja na mfumo wao kama ilivyokuwa kwa Simba, tutakuwa tunabadilika kwa kuangalia mazingira ya mchezo unavyokwenda, ” Pluijm alisema.
Kukosekana kwa Niyonzima na Twite huenda Mholanzi huyo akawaanzisha viungo Salum Telela na Juma Abdul katika mechi hiyo ambayo Mecky, Mexime, Kocha wa Mtibwa Sugar, ametamba kwamba anaijua ‘dawa’ ya Yanga.
Mexime alisema kuwa timu yake haina wasiwasi yoyote katika mchezo huo na kusema kwamba wamejipanga kuisimamisha Yanga na hatimaye kushika usukani wa ligi.
“Naijua Yanga ni timu kubwa lakini naamini timu yangu ni nzuri na wasitarajie mteremko kwenye mchezo wa kesho (leo),”alisema beki huyo wa zamani wa Mtibwa Sugar na Taifa Stars.
Kocha Mkuu wa Simba, Dylan Kerr, alisema jana kuwa wachezaji wake wanapaswa kusahau matokeo ya mchezo uliopita na kuelekeza akili zao kwenye mchezo wa leo na kusahau kichapo cha mabao 2-0 kutoka kwa mahasimu wao Yanga.
“Ligi bado mbichi huwezi kujua kitakachotokea mbele, tumepoteza mchezo dhidi ya Yanga na hilo limepita, nataka tuingie uwanjani kesho (leo) huku tukielekeza akili zetu kwenye mchezo huo, ushindi utaturudisha kwenye mstari,” alisema Kerr.
Mechi nyingine za ligi hiyo zinazotarajiwa kufanyika leo ni kati ya Azam FC watakaoikaribisha Coastal Union kutoka Tanga huku Majimaji wakiwa wenyeji wa Ndanda FC mjini Songea na Kagera Sugar inayotumia Uwanja wa Ali Hasan Mwinyi mkoani Tabora watacheza na  JKT Ruvu ya Pwani.
African Sport wataivaa Mgambo JKT kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga,  wakati Tanzania Prisons watacheza na Mwadui huku kesho Alhamisi Toto Africana wakiikaribisha Mbeya City kwenye Uwanja wa CCM Kirumba Mwanza.
CHANZO: NIPASHE






Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: