BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

JE WAJUA CHANGAMOTO ZA NDOA ZA VIJANA


Kuna baadhi ya nchi ambako wavulana na wasichana wengi wameingia katika ndoa. Hii ni hali ambayo tunaweza kuiita mbio za vijana kukimbilia katika ndoa. 


Tunapotafakari kuna swali ambalo wataalamu wa saikilojia wanajiuliza. Je, ni vyema kwa vijana wa umri wa kati ya miaka 18 – 19 hukimbilia kwenye ndoa?

Hebu tuanze kwa kujiuliza “Je, msichana anayechukua muda mrefu kuchagua kwa makini mume atakayemfaa ana fursa ya kumpata anayefaa zaidi kuliko yule ambaye hapotezi muda? Yaani mara moja tu huweza kumpata mume huyo.

Aidha, tunawaza nini kuhusu mvulana anayetembelea maduka mengi ili kupata shati zuri au yule anayeingia katika duka la kwanza na la pili kisha kuamini kuwa amepata bahati ya kuona shati ambalo anafikiria ni zuri. 


Yule anayechukua muda wa kutosha huweza kupata nguo nzuri na bora zaidi kuliko yule ambaye anapoiona nguo fulani ikamvutia mara anahisi kuwa ndiyo inayomfaa zaidi na kuamua kuichukua.

Ingawa imepita miaka mingi na huenda sikumbuki vizuri, mimi nilimchagua mchumba kwa miaka mingi nikampata nilipokuwa na miaka 26. 


Kutokana na uzoefu wangu na hali ninayoiona katika zama hizi tulizonazo ninashawishika kufikiri kuwa, wasichana na wavulana wa siku hizi wanaotamani kuingia katika ndoa wakiwa wangali vijana wadogo, wangeweza kuwa na ndoa za furaha zaidi kama wangekuwa na subira zaidi kidogo.

Kuna baadhi ya vijana wenye hisia hizi, ninapowashauri wafanye subira hunipinga kwa kusema, “Ni vyema zaidi kupata watoto ukiwa ungali kijana mdogo kuliko kusubiri hadi ukawa na umri mkubwa.” 


Lakini mimi huwa nahisi tunaposema mzazi, mama au baba anapaswa kuonekana mzazi kweli. Isiwe anapojumuika na wanawe wanaonekana kama kikundi tu cha maskauti wa kike au kiume wenye rika moja.

Lakini vile vile kuna wazazi wanaonipinga kwa hoja kuwa ndoa za vijana wadogo zina manufaa sana kwa sababu ndiyo dawa pekee ya kuepuka tabia ya ngono nje ya ndoa na mimba za utotoni.

Ingawa wakati mwingine ninatamani kuafikiana na hoja zao lakini nashindwa kabisa kuamini kuwa ngono nje ya ndoa inawahusu zaidi vijana wadogo. Bado tabia zinazokwenda kinyume na maadili, hususan kuhusu mapenzi, ndoa na ngono ni suala ambalo wazazi tuna wajibu nalo mkubwa na hatuna sababu ya kujaribu kutafuta njia ya mkato ya kukwepa majukumu ya dhamana yetu kwa watoto wetu.

Wakati mwingine ninapowafikiria watu wazima ambao ni mawakili wa ndoa za vijana wadogo, nashindwa kuelewa wanawezaje kufikiria kuwa vijana wanaweza kujifunza wenyewe maadili ya mapenzi, ngono na ndoa watakapoana wakiwa katika umri mdogo.

Kwa kawaida wanapoona kila mmoja anaondoka kwenye himaya ya wazazi wake na wao wawili wanaamua kuanza kujenga kaya yao wenyewe huku wakiwa na wajibu mkubwa zaidi. Kwa dhamana kubwa ambayo kila mwanandoa huwa anayo napaona hapa ndipo hoja yangu kuhusu ndoa za vijana inapopata mashiko.

Kadri vijana wanavyo subiri wakakua zaidi ndivyo kadri wanavyojipa nafasi ya kukomaa kiakili wakaweza kuchagua mshirika anayefaa zaidi. Sifa za ujana kama vile ulimbwende kwa msichama na utamashati kwa mvulana hazina thamani katika ndoa zikilinganishwa na sifa nyingine kama vile ukarimu, ucheshi, heshima na upendo ambazo ndizo sifa muhimu kwa mwenza wa ndoa kuwa nazo. 


Kadri kijana anavyokua ndivyo anavyotoka taratibu katika hali ya kuthamini urembo, mapambo na nakshi zinazompamba mtu.

Licha ya sifa hizi nilizozitaja kuna suala jingine ambalo hutawala akili za kijana. Kila mmoja huwa na matarajio na matumaini makubwa zaidi kuliko hali halisi ilivyo. Mvulana humtazama mchumba wake kama malikia na msichana naye humuona mchumba wake kama handsome boy wote wawili huwa na shauku ya shani kubwa watakapooana. 


Lakini wanapoingia katika ndoa mambo yale waliyoyaona yana thamani ugundua hayana maana yoyote katika maisha halisi ya ndoa.

Vijana wadogo wanapoona yale waliyokuwa wameyatarajia katika ndoa hayatokei huwa wanapata mshituko ambao huweza kuiyumbisha ndoa. Hata hivyo, kwa vijana waliokomaaa kidogo huwa wana busara na uvumilivu na huweza kujirekebisha ili ndoa yao idumu.

Kukosekana kwa busara na ustahamilivu unaotakiwa katika maisha huweza kusababisha ndoa kuvunjika. Hili linapotokea katika ndoa za ujanani haifai kufikiriwa kuwa ni udhaifu wa tabia, kwani ni hali halisi ya kimaumbile. Ndoa ya vijana wadogo ni kama mti ambao haujakomaa maana hauwezi kubeba mzigo mzito.

Kuna kisa cha wanandoa wawili wadogo. Mume alikuwa na miaka 20 na mke miaka 18. Baada ya mume kufukuzwa kazi kutokana na kutokuwa makini zaidi, mkewe alikimbilia nyumbani kwa wazazi wake. Alipoulizwa na wazazi wake kwa nini amefanya hivyo, alisema ameondoka kwa mumewe ili asiwe mzigo kwake wakati hana kazi. 


Wazazi wa pande zote mbili walikubaliana kuwa kutokana na umri wake hakuwa ni mwanamke wa makamu ya kuweza kustahamili. Kama angekuwa ameolewa baada ya miaka mitano hadi sita, angeamua kubaki na mumewe ili washirikiane na kushauriana jambo la kufanya ili kulikabili tatizo hilo pamoja na maisha yaendelee.

Kuna sababu nyingine inayonifanya nishauri vijana wasubiri kidogo kabla ya kuingia katika ndoa. Wanapokomaa zaidi wanakuwa wamepata uwezo wa kujitegemea katika uwezo wa kufanya uamuzi yao wenyewe. Kuna tabia waliyonayo vijana wadogo hususan wasichana.

Huwa wanapenda kuegemea zaidi kwa wazazi wao ili kupata ushauri hata wanapokuwa wameolewa. Kwa mwenendo huu kuna hatari kuwa ndoa za vijana huweza kuendeshwa na wakwe.

Yaani mke anamweleza mumewe jinsi wazazi wake wanavyotaka wafanye katika ndoa yao na mwanamume naye anamuamrisha mkewe afanye kama wazazi wake wanavyotaka.

Hapana shaka ndoa kama hii itayumba kwa sababu itakuwa kama chombo cha baharini kinachoendeshwa na mabaharia mawili.Mwananchi
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: