BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

DK SLAA AWAONYESHA WATANZANIA RAIS ANAYEFAA KUCHAGULIWA OKTOBA 25 MWAKA HUU, LAKINI USALAMA WA TAIFA WALAZIMIKA KUMLINDA.

 
Dk Slaa: Ninalindwa na Usalama wa Taifa

Dar es Salaam.
Katibu mkuu wa zamani wa Chadema, Dk Willibrod Slaa juzi alijitokeza tena hadharani kujibu mapigo ya hoja mbalimbali zilizojitokeza wakati akitangaza kustaafu siasa za vyama, akiweka bayana kwamba hivi sasa analindwa na usalama na amehama nyumbani kwake.

Dk Slaa alitangaza kujiondoa kwenye siasa za vyama Septemba mosi, akieleza kuwa alitofautiana na viongozi wenzake wa Chadema kuhusu namna ya kumpokea Edward Lowassa kutoka CCM ili awe mwanachama na mgombea urais, na akatumia fursa hiyo kumrushia ‘makombora’ mgombea huyo wa urais kwa tiketi ya Ukawa.

Hotuba yake ilizua maswali mengi, ikiwa ni pamoja na gharama alizotumia kurusha moja kwa moja mkutano na wake na waandishi wa habari kwenye Hoteli ya Serena, huku mkewe wa zamani akijitokeza kukanusha kuishi maisha ya shida, huku Ukawa ikisema alikuwa akiutaka urais, tofauti na maelezo yake.

Akihojiwa kwenye kipindi maalumu kilichorushwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha Star Tv juzi usiku, Dk Slaa alisema sambamba na kuhamia Hoteli ya Serena, ambayo ni ya kiwango cha nyota tano, hata nyumba yake inalindwa na usalama wa taifa.

“Nakaa Serena kwa sababu ninapata vitisho, nilishasema kuwa kipindi hiki nimepata vitisho vingi kuliko nilivyopata wakati nilipotaja orodha ya mafisadi. Watanzania hawajui jinsi mimi na familia yangu tunavyoishi,” alisema.

Katika mazungumzo yake na Star Tv yaliyodumu kwa dakika 85, Dk Slaa alisema amekuwa akipata vitisho vingi, vinavyoiweka familia yake hatarini huku akieleza jinsi mke wake, Josephine Mushumbusi alivyokoswakoswa na risasi akiwa kwenye gari.

“Si ajabu mimi kulindwa na Usalama wa Taifa. Ingawa nilishawahi kuwasema hawa watu wa usalama, sasa wananilinda na ni utaratibu kuwa ukiomba ulinzi kwa utaratibu unaotakiwa, unapewa,” alisema.

Alifafanua zaidi kuwa ameshtushwa na uzushi ulionezwa kuwa amekimbilia Marekani, akisema hajawahi kufanya hivyo, bali aliwahi kwenda nchini humo mwaka jana katika kazi zake za siasa.

“Niliwahi kwenda Marekani mwaka jana katika kazi zangu za siasa na nikatembelea majimbo 13. Gharama hizo nilijilipia mwenyewe, nilikwenda kujifunza mambo fulani fulani ya uongozi,” alisema.

Amjibu Lissu, Kamili
Dk Slaa alitumia wasaa huo kumjibu mnadhimu na mwanasheria mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, akisema yeye ni mstaarabu na hawezi kuzungumza mambo ya kumchafua mbunge huyo wa Singida Mashariki.

“Ningetaka kuongea mambo ya familia ya Lissu, ningeongea, lakini mimi ni mstaarabu. Tuna watu tunaodhani ni wasomi lakini usomi wao hauonekani,” alisema.

Saa chache baada ya Dk Slaa kuzungumza na wanahabari Septemba Mosi, Lissu alihojiwa na kituo cha redio cha Marekani(VOA) na kusema kuwa Dk Slaa anastaafu chama wakati bado anapokea mshahara, anaendesha gari la chama na nyumba anayoishi alinunuliwa na chama.

Lakini Dk Slaa alisema alianza kuwalipa walinzi mwezi mmoja uliopita, na hajachukua mshahara wake na kuwa gari la chama alikwishalirudisha.

Katibu huyo wa zamani wa Chadema alizidi kupangua hoja hizo moja baada ya nyingine huku Star Tv ikirejea baadhi ya sauti za watu waliozungumza kama Lissu na mwenyekiti mwenza wa Ukawa, James Mbatia.

Kadhalika Dk Slaa alimjibu mke wake wa zamani, Rose Kamili ambaye alikanusha kauli ya katibu huyo wa zamani wa Chadema kuwa wanaishi kwa kula mihogo kwa ajili ya kulitumikia Taifa.

Dk Slaa alikanusha kuitelekeza familia hiyo na kusema kuwa watoto aliozaa na Kamili ni wakubwa, ambao wana uwezo wa kujitegemea.

“Niliposema kuhusu mihogo sikuzungumzia watu wazima, ukifikisha miaka 25 bado unalelewa na wazazi? Watoto ni watu wazima na wana watoto na wanafamilia zao, bado walelewe?” alisema.

Kuhusu kuonekana na Mwakyembe
Akiendelea kupangua hoja hizo na wakati mwingine akithibitisha uvumi ulionea kwenye mitandao ya kijamii, Dk Slaa alikiri kuonekana na Waziri wa Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe katika hoteli ya Serena saa chache kabla ya mkutano wake na wanahabari Septemba Mosi.

Dk Slaa alisema alionana na Dk Mwakyembe ili kupata hadidu za rejea kuhusu kesi ya Richmond, kwa kuwa mbunge huyo wa Kyela alikuwa mwenyekiti wa Kamati ya Uchunguzi kuhusu sakata hilo mwaka 2007.

“Kwenye kufanya utafiti, kuna kitu kinaitwa ‘research methodology’ (mbinu za utafiti), na mimi nilikutana na Mwakyembe ili kutafuta taarifa kabla sijazungumza na wanahabari,” alisema Dk Slaa ambaye amekuwa akihubiri ufisadi wa Richmond tangu mwaka 2008.

“Mimi siyumbishwi, nimetimiza wajibu wangu kwa nafasi yangu na kwa dhamira yangu, nimetimiza wajibu wangu kwa Taifa langu,” alisema.

Kuhusu kutumiwa na CCM
Katibu huyo mstaafu alitumia nafasi hiyo kujibu tetesi zinazoendelea kuvuma kuwa anatumiwa na CCM kuuvuruga Ukawa, akisema kuwa ana uwezo wa kisiasa wa kutenganisha mambo na hawezi kutumiwa.

“Mbona hamkusema chochote nilipokwenda na Rais Jakaya Kikwete kwenye harambee ya CCBRT? Niliongozana naye na tulitembea kwa miguu kutoka Golden Tulip, mbona hamkusema,” alisema.

“Hoja zao ni dhaifu watu hao hawajui kupambanua siasa na maendeleo.”

Dk Slaa alipoulizwa kuhusu Rais ajaye, alisema swali hilo ni gumu, lakini akaeleza kuwa Watanzania wanatakiwa wachague Rais asiye na upungufu na kuwataka waache ushabiki.

Alisema Lowassa anayewania urais chini ya mwamvuli wa Ukawa na John Magufuli wa CCM wote wana upungufu, lakini kuna mmoja ana upungufu zaidi.

“Katika vitu viwili vibovu unaangalia kipi ni kibovu zaidi na unachagua kile chenye unafuu,” alisema.CHANZO:MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: