BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

MADAWA YA KULEVYA: ASKOFU JOSEPHAT GWAJIMA APALEKWA KUSIKOJULIKANA NA POLISI

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam jana lilimpeleka Askofu Josephat Gwajima kusikojulikana baada ya waumini wa kanisa lake la Ufufuo na Uzima kufurika katika Kituo Kikuu cha Kati, jijini.

Gwajima ambaye alikuwa amefika kituoni hapo siku moja kabla ya tarehe ya wito, aliondolewa Kituo Kikuu cha Kati saa 10:27 jioni baada ya kupandishwa kwenye gari aina ya Toyota Land Cruiser.

Gari hiyo inayodaiwa ni ya usalama, iliondoka na Gwajima ambaye juzi Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alimtaja katika orodha ya watu 65 ambao anataka walisaidie dola kuhusu biashara ya madawa ya kulevya.

Mbali na kiongozi huyo wa dini, orodha hiyo pia ilikuwa na wafanyabiashara na wanasiasa.

Licha ya Gwajima kuchukuliwa kutoka kituoni hapo maeneo ya Stesheni, wafuasi wake waliendelea kupiga kambi katika eneo hilo.

Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Simon Sirro, alisema atatoa leo taarifa kuhusiana na alikopelekwa Askofu Gwajima, baada ya kuulizwa na Nipashe kwa simu jana.

Awali Gwajima alifika kituoni hapo saa 7:32 mchana akiwa katika gari aina ya Hummer lenye namba za usajili T427 CYV na kuelekea katika kituo hicho cha polisi kwa lengo la kuitikia wito huo.

Mchungaji Gwajima aliingia kituoni hapo akiwa ameongozana na watu watatu.

Ndani ya muda mfupi baadaye waumini wake waliokuwa wamevalia suti nyeusi na mashati au blauzi nyekundu walimiminika na kukusanyika pamoja nje ya kituo hicho.

Polisi iliwafukuza na kuwataka kutawanyika lakini walisogea pembeni kidogo na kuweka kambi. Wengine walivuka barabara na kusimama Stesheni ya treni.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi, Makonda aliwataka wote 65 aliowataja kujisalimisha Polisi leo kwa ajili ya mahojiano na kwamba miongoni mwao wamo wanaojihusisha na uuzaji, wanaotumia na wenye taarifa za kuwezesha Jeshi la Polisi kuupata mtandao mzima wa dawa za kulevya.

“Awamu hii ya pili haitakuwa nyepesi kwa sababu itakuwa na mawimbi mengi ambayo naamini Rais John Magufuli, ambaye ndiye nahodha wa meli hii ataivusha salama Tanzania baada ya kumaliza uongozi wake kwenye vita ya dawa za kulevya,” alisema Makonda. 


Katika awamu yake ya kwanza ya vita dhidi ya madawa ya kulevya, Makonda alitaja orodha ya wasanii na askari polisi 12 aliowaita pia kwa sababu hizo.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: