BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

RC MAKONDA AFYATA MKIA KWA KUONYESHA UNYENYEKEVU MKUBWA MBELE YA BUNGE


PAMOJA na majigambo na lugha za kejeli, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, amesalimu amri mbele ya Bunge na hatimaye chombo hicho kumsamehe baada ya kuomba radhi na kuonyesha unyenyekevu, alipoitwa kuhojiwa.

Mbali na kiongozi huyo, bunge pia limewasamehe Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe na Mkuu wa Wilaya Arumeru, Alexander Mnyeti, baada ya kufuata nyayo za Makonda kwa kukiri kutekeleza na kuomba radhi kwa kutoa lugha isiyofaa.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, Almas Maige akiwasilisha bungeni mjini hapa jana taarifa kuhusu mashauri yanayowahusu watatu hao, alipendekeza Bunge liwasamehe kutokana na uungwana wao wa kukiri, kuomba radhi na kujutia makosa yao walipofika mbele ya kamati hiyo kwa ajili ya kuhojiwa.

Akizungumzia shauri la kigogo huyo, aliyekuwa anatuhumiwa kusema wabunge wanasinzia bungeni, Maige alisema kamati yake ilikuwa na hadidu mbili za rejea, kama ni kweli alitamka maneno hayo yaliyolalamikiwa na wabunge na hatua za kisheria zinazopaswa kuchukuliwa dhidi ya yake kama alitenda kosa hilo.

Alisema chanzo cha malalamiko dhidi yake ni hatua aliyoichukua ya kutaja majina ya watu wanaojihusisha na dawa za kulevya.

Alisema katika mkutano wake na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam, kiongozi huyo wa serikali aliulizwa hatua anazozichukua dhidi ya baadhi ya wabunge wanaotuhumiwa kujihusisha na dawa za kulevya na wengine walikuwa wameanza kutajana wao wenyewe bungeni.

Kwa mujibu wa Maige, katika kujibu swali hilo, alisema: "... zingine ni mbwembwe tu, unajua mle ndani (bungeni) wakati mwingine wanachoka na kusinzia lazima kuwe na watu kidogo akili zao zinawasaidia kuamka, kucheka na kufurahi maisha yanaendelea."

Maige alisema kiongozi huyo alifika mbele ya kamati yake Machi 29, mwaka huu, majira ya saa nne asubuhi kwenye Ukumbi wa Spika na kusomewa tuhuma dhidi yake na kukiri kwamba ni kweli alitoa kauli hiyo.

Alisema katika maelezo yake alionyesha kujutia kauli hiyo ambayo iliwakwaza na kuwavunjia heshima wabunge, hivyo aliomba radhi na kueleza kuwa hata kabla ya kuitwa mbele ya kamati, tayari alikuwa ameandika barua kwa Spika ya kuliomba radhi Bunge.

Maige alinukuu sehemu ya maelezo ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kuomba radhi kuwa ni: "... najisikia vibaya kusimama mbele yenu kwa kuwakwaza na kuwavunjia heshima ambayo sikupaswa kufanya hasa kwa watu ambao mmekuwa walezi na ni watu ambao mnanitegemea nifanye vizuri kwa ajili ya kuwawakilisha vijana wengine.

"Itakumbukwa baada ya kauli yangu, nilichukua jukumu la kuandika barua kwa Mheshimiwa Spika, baada ya kusikiliza mjadala katika Bunge na kumwomba radhi kwa kitendo cha kauli yangu niliyoitoa wakati nikijibu swali pale ambapo mwandishi alitaka kujua mambo kadhaa yaliyofanyika.

"Kwa hiyo, akili yangu ilikuwa na mtazamo wa namna hiyo, haikuwa na mtazamo wa kulidharau Bunge, haikuwa na mtazamo wa kumvunjia heshima mbunge yeyote yule na kwa kweli najisikia vibaya sana kusimama mbele yenu na ninaomba radhi sana sana kwa kauli niliyoitoa na tafsiri iliyopatikana."

Kutokana na maelezo hayo, Maige alisema kamati yake imejiridhisha bila shaka yoyote kwamba maneno ya Mkuu wa Mkoa huyo yalivunja haki na kudharau mamlaka ya Bunge.

Alisema kitendo cha kutamka maneno hayo ni cha kudharau, kudhalilisha na kulifedhehesha Bunge.

Hata hivyo, licha ya kukiuka masharti ya kifungu cha 26(e) cha Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge (Sura ya 296), Maige alisema Bunge limeazimia Mkuu wa Mkoa huyo asamehewe kutokana na kitendo chake cha kiungwana cha kukiri na kujutia kosa lake na kuliomba radhi Bunge mbele ya kamati yake.

Alisema kamati yake imezingatia ukweli kwamba Mkuu wa Mkoa huyo hakuisumbua kwa namna yoyote ile bali alikuwa mtii na alitoa ushirikiano mkubwa kwa kamati.

Alisema kamati pia imezingatia kuwa kiongozi huyo wa serikali hakuwa na dhamira ya kulidharau wala kulidhalilisha Bunge kama ambavyo ilichukuliwa.

Mbunge huyo wa Newala (CCM) alisema kamati imezingatia kuwa Mkuu wa Mkoa huyo alikuwa hajawahi kutenda kosa kama hilo na kufikishwa mbele ya kamati na pia amekiri kosa lake na kuomba radhi.

Alisema msamaha wake pia umezingatia kitendo cha Mkuu wa Mkoa huyo kuandika barua kwa Spika kuomba radhi, uzoefu wa mabunge mengine ya Jumuiya ya Madola kuhusu adhabu kwa mtu ambaye amekiri kosa la kudharau Bunge na kuomba msamaha.

SHAURI DC MNYETI
Akizungumzia shauri la DC Mnyeti, Maige alisema chanzo cha malalamiko hayo ni taarifa ya Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa iliyowasilishwa Februari 3, mwaka huu na kuanisha changamoto za mapendekezo ya kuzitatua ikiwa ni pamoja na suala la Wakuu wa Mikoa na Wilaya kutumia vibaya mamlaka yao.

Maige alisema kuwa katika taarifa hiyo, kamati ilipendekeza waziri mwenye dhamana awapatie semina viongozi hao wa serikali namna ya kutekeleza majukumu yao.

Kutokana na masuala mbalimbali yaliyojadiliwa bungeni kuhusiana na jambo hilo, Maige alisema ndipo Mnyeti alipoandika katika ukurasa wake wa mtandao wa Facebook akiyaita mapendekezo hayo ni ya upuuzi mtupu na kwama wabunge hawajielewi na anawashauri wafanye kazi zao.

Akinukuu maneno hayo, Maige alisema: "Upuuzi mtupu. Wabunge hawa hawajielewi. Nawashauri fanyeni kazi zenu za wengine waachie wenyewe."

Alisema kuwa Mnyeti aliitwa mbele ya kamati hiyo Aprili 6, mwaka huu na kuhojiwa kuhusu tuhuma zilizomkabili na alikiri kuandika maneno hayo na kumiliki akaunti ya Facebook iliyoandika maneno yaliyolalamikiwa.

Alisema kuwa baada ya maelezo, shahidi aliomba radhi kwa Bunge na kusema hana ubavu wa kushindana nalo.

Maige alinukuu maneno ya Mnyeti akisema: "...Mheshimiwa Mwenyekiti, basi naomba sasa kamati yako itumie busara na ninaomba radhi kwamba limekuwa kubwa lakini halikuwa kusudio langu tangu awali kwamba sasa nilikwaze Bunge kwa 'style' (mtindo) hiyo.

"Mimi naomba radhi kamati yako, itumie busara zake lakini lengo kutoka moyoni kwangu halikuwa katika hali hiyo ambayo limechukuliwa... Nikiri kuwa ni madhaifu yangu sikutenda kiungwana, naomba kamati inisamehe kuanzia sasa na kuendelea haitajirudia tena. Kwa hiyo, binafsi niiombe kamati yako kwa nafasi ya kipekee ione umuhimu wa kunisamehe..."

Kutokana na maelezo hayo ya Mnyeti, Mkuchika alisema kamati yake imethibitisha kuwa Mkuu wa Wilaya huyo aliingilia uhuru na kuvunja haki za Bunge kinyume cha kifungu cha 26(e) cha Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge.

Alisema kitendo cha kuandika maneno hayo ni cha dharau, kudhalilisha na kulifedhehesha Bunge lakini kwa kuzingatia kwamba Mnyeti hakuisumbua kamati na alikuwa mtii na kutoa ushirikiano na hajawahi kutenda kosa jingine la aina hiyo, Bunge limeazimia kumsamehe.

Februari 8, mwaka huu, Bunge lilipitisha maazimio ya kuwaita bungeni na kuwahoji Makonda na Mnyeti kutokana na hoja ya Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara (Chadema) aliyewatuhumu viongozi hao wa serikali kuudharau mhimili huo na ikithibitika, wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria zilizopo.

SHAURI LA MBOWE
Akizungumzia shauri la Mbowe, Mkuchika alisema lilianzia Aprili 4, mwaka huu wakati wa mkutano wa kwanza wa Bunge la Bajeti ambao ulikuwa na uchaguzi wa wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) ambapo baadhi ya wabunge walionekana kufanya vitendo vya utovu wa nidhamu.

Alisema Mbowe alinukuliwa na vyombo vya habari akitoa maneno ya utovu wa nidhamu kwa kudharau Mamlaka ya Spika na kutoa maneno ya kuudhi dhidi ya wabunge wengine, kitendo ambacho alikifanya akiwa nje ya ukumbi wa Bunge baada ya uchaguzi huo.

Katika uchunguzi wa kamati yake, Mkuchika alisema walijiridhisha kuwa Mbowe alitamka maneno: "... Spika amevunja Kanuni za Bunge, sheria hazikuheshimiwa, ubabe umetumika... ni mkakati wa kiserikali, tunajua Rais anahusika, Waziri Mkuu anahusika, viongozi wa chama chao wanahusika...

"...tumeleta wagombea wazuri sana wawili 'very competent', wamepigiwa kura za hapana kwa sababu ulikuwa mkakati wa Chama Cha Mapinduzi, tumeona ujinga na upumbavu mtupu... uchaguzi huu umekuwa wa kijinga"

Mkuchika alisema kuwa baada ya kumuita mbele ya kamati, Mbowe alikiri wazi kuwa alitamka maneno hayo na akaliomba radhi Bunge.

Licha ya kumtia hatiani kiongozi huyo wa upinzani kwa kudharau mamlaka ya Spika, Mkuchika alisema Bunge limeazimia kumsamehe kutokana na kitendo chake cha kuonyesha ushirikiano na kuomba radhi huku likimkumbusha kuwa anatakiwa kuwa mfano kwa wengine anaowaongoza. 


Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Mbunge wa Hai, alitakiwa na Spika kufika mbele ya kamati hiyo mwanzoni mwa mwezi uliopita baada ya Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM) kulamika bungeni kuhusu kauli zake hizo zilizomtia hatiani.Nipashe
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: