BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

BOSI WA WAENDESHA BODABODA AJINYONGA KWA KUTUMIA WAYA WA SIMU SHINYANGA

 
SIKU chache tu baada ya waendesha bodaboda kutawanywa kwa mabomu na polisi wakidai wamesababisha kifo cha mwenzao, Mwenyekiti wa Chama cha Waendesha Pikipiki wa Manispaa ya Shinyanga, Jacob Paul (36) amekutwa amejinyonga kwa kutumia waya wa simu.

Taarifa zilizopatikana mjini Shinyanga hivi karibuni na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Jumanne Muliro zilisema tukio hilo lilitokea saa 8 mchana akiwa chumbani kwake Mtaa wa Mwinamila Kata ya Ngokolo Manispaa ya Shinyanga.

Kwa mujibu wa Sarah Edward, mwenyekiti huyo wa waendesha bodaboda alifika nyumbani kwake saa 7 mchana akiwa amepakizwa na mwendesha bodaboda mwenzake kisha kuingia ndani kwake na mwendesha bodaboda huyo akaondoka.

“Baada ya dakika 30 hivi, watoto wa mwenyekiti huyo walifika nyumbani wakitaka kuingia ndani lakini mlango wa nyumba ulikuwa umefungwa.

“Walipochungulia dirishani walimuona baba yao akiwa amening’inia chumbani, waliomba msaada kwa majirani na baadaye taarifa polisi,” alisema.

Kutokana na hali hiyo waliamua kuvunja mlangona kukuta akiwa amejinyonga.

Kujiua kwa mwenyekiti huyo wa waendesha bodaboda kumetokea siku chache baada ya Joel Gabriel Mamla (26), kufariki dunia wakati akiwa amekamatwa na polisi.

Hali hiyo ilisababisha vurugu baada ya waendersha bodaboda kuandamana na kutawanywa na polisi kwa mabomu ya machozi.

Mke wa mwenyekiti huyo, Rebecca Amos, alidai kifo cha mume wake kimetokana na masuala ya bodaboda na siyo jambo jingine.

Naye Diwani wa Kata ya Ngokolo, Emmanuel Ntobi (CCM), alieleza kusikitishwa na tukio hilo na kumuomba Rais Dk. John Magufuli kuunda tume huru ya kufuatilia na kuchunguza vifo vya waendesha bodaboda katika Manispaa ya Shinyanga.

“Sasa ni vifo viwili vya waendesha bodaboda vimetokea… jamii inasema vinasababishwa na polisi wenyewe na wao wanadai wao ndiyo wanaosababisha vifo vyao kwa kukiuka sheria za usalama barabarani.

“Inaonekana ameamua kujiua kutokana na msongo wa mawazo, akilinganisha na matukio ya wenzake wawili kupoteza maisha huku wenzake wakimlaumu na mpaka sasa pikipiki nyingi za waendesha bodaboda zimekamatwa na wengine wanashikiliwa na polisi,” alisema Ntobi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Jumanne Muliro alithibitisha tukio hilo.

Alisema mwenyekiti huyo alikutwa akiwa amejinyonga kwa waya mgumu wa simu katika chumba chake.

“Tumekuta amefariki dunia kwa kujinyonga.

“Kwa mujibu wa baba mwenye nyumba hiyo, watoto wake wawili walikuta mlango umefungwa na walipochungulia wakamuona baba yao amening’inia chini kuna dumu la maji pembeni mwa kitanda chake,”alisema.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: