BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

ZAMA ZA UTAWALA WA RAIS WA ZAIRE MOBUTU SESESEKO NA MISUKOSUKO KIBAO



Kuzaliwa 14 October 1930
KUFA 7 September 1997, Rabat, Morocco
Jina halisi Joseph Desire Mobutu.

Na
Kizito Makoye
Mobutu Seseseko alizaliwa na kujulikana kama Joseph Mobutu hukoS Kongo wakati huo ikiitwa Leopoldvile. Baba yake alikuwa mpishi, aliyekufa wakati Mobutu akiwa mtoto,na mama yake alikuwa mhudumu wa hotel. 

Alitumia kipato chake kumsomesha shule ya mabruda(brothers) ya Kikatoliki. Mwaka 1949 alijiunga na jeshi lililojulikana kama (Force Publique) Kikundi cha wanausalama wa Kongo walioongozwa na askari wa Ubelgiji, na akapanda cheo mpaka kuwa sajenti. 

Alibaki jeshini kwa miaka saba, huku akiwa jeshini alifanya kazi kama mwandishi wa habari na kuchangia Makala kwenye magazeti huko Leopoldville( Kinshasa. Na alivyaacha kazi jeshini alikuwa ripota kwenye gazeti la kila siku la L’Avenir( The Future) na baadae Mhariri wa Gazeti la Actualites Africaines.

Ni katika nafasi hiyo ya uandishi wa habari ndipo alipokutana na mwana mapinduzi Patrice Lumumba, na Mobutu alivutiwa sana nae kiasi cha kujiunga na chama chake cha Vuguvugu la kitaifa la kongo( Congolese National Movement (MNC).


Kongo ilipopata uhuru mwaka 1960, serikali ya umoja wa kitaifa iliundwa, Lumumba akiwa Waziri Mkuu na Joseph Kasavubu kama Rais. Mobutu aliteuliwa kuwa mnadhimu mkuu wa Jeshi. 


Baadae Lumumba na Kasavubu wakakosana wakigombania madaraka, na September 14, 1960, askari waasi jeshini wakampindua Lumumba na kumweka Kasavubu kama kiongozi wa ujumla. Mmoja ya watu walioshiriki mapindizi hayo hakuwa mwingine ila ni rafiki wa zamani wa Lumumba—Mobutu. 
Ilijulikana baadae shirika la ujasusi la marekani CIA na serikali ya Ubelgiji wote hawakumwamini Lumumba, baada ya kumuhisi kuwa ni mkomunisti, au walau anatetea sera za ukomunisti, na wakamtaka Kasavubu awe madarakani, kama walivyoamini na ndivyo ilivyokuwa, Kasavubu na Mobutu wangalikuwa rahisi kutumiwa. 

Miaka mitano baadaye, hata hivyo Mobutu aliongoza jaribio lingine la mapinduzi dhidi ya Kasavubu, ambaye alishinda jaribio kama hilo dhidi ya mpinzani wake mwenye kupendwa, waziri mkuu Moise Tshombe. 


Baada ya kunyakua madaraka, Mobutu alikataza vyama vya kisiasa na kuamuru hali ya hatari, na kuhodhi mamlaka kamili ya kiongozi dharimu( dictator). Baadae alianzisha chama chake mwenyewe, kilichojulikana kama vuguvugu maarufu la mapinduzi (Popular Movement of the Revolution), ambacho wakongomani wote walipaswa kujiunga nacho.

Aliamuru vyama vya wafanyakazi kuanzisha Umoja wa kitaifa wa wafanyakazi wa Zaire , na kukiweka chini ya uongozi wa serikali.
Ingawa kulikuwa na majaribio mengi dhidi ya utawala wake, yote yalizimwa kwa ukatili wa hali ya juu. 


Mwaka 1970, Mobutu alifanya uchaguzi ambao alikuwa mgombea pekee na ambapo kupiga kura ilikuwa ni lazima. Bila mshangao, alipata asilimia 99 ya kura. 

Mwaka 1971 alianzisha mpango wa kujitambua na utamaduni na kubadili jina la nchi Jamhuri ya Zaire. Aliamuru wakongomani wenye majina ya kikristo kuyaacha na kuchukua majina ya Kiafrika, ubatizo wa watoto ulikatazwa na mfumo ya maisha ya kimagharibi ulikatazwa na ufungaji tai zilizuiwa. 

Mwaka uliofuata alijiita mwenyewe Mobutu Seseseko Kuku Nbendu wa Zabanga, hata hivyo ili kurahisisha aliruhusu aitwe Mobutu Sese Seko.
Alihodhi taswira binafsi( personality cult) ambapo picha zake zilionekana popote na kwenye kila kitu kuanzia stempu za posta hadi kwenye noti.


Alama pekee aliyoichagua kiasi cha kuwa kielelezo cha utawala wake ni kofia iliyoshonwa kwa mkono yenye ngozi ya chui, fimbo iliyochongwa na umbile la kichwa cha mwewe kwa juu.


Utawala wake dharimu na wa mabavu ulisababisha majaribio mengi ya kijeshi dhidi yake hata hivyo suluhu pekee ilikuwa ni kufanya mauaji ya halaiki kwa wapinzani wake wa kweli na wa kuhisi na kujikuta kwenye matatizo kidogo licha ya kupata taswira mbaya sana duniani.


Alitaifisha makampuni ya kimataifa na kuwafukuza wamiliki wake wazungu na mameneja. Aliyakabidhi makampuni hayo kwa ndugu zake wa karibu na washirika wa kisiasa, wengi wao walifuja mali za makampuni hayo. 


Hali mbaya ya kiuchumi kutokana na hatua hiyo ilimlazimu Mobutu kuwarudisha wazungu mwaka 1977. Mwaka huo huo kikundi cha waasi—wafuasi wa Tshombe aliyeuwawa na Mobutu walivamia jimbo la Katanga kutoka kwenye kambi yao nchini Angola.

Walikuwa na mafunzo ya hali ya juu, motisha huku wakiongozwa na mamluki wenye weledi kutoka Afrika ya Kusini na Ulaya, walifanikiwa kuliswaga jeshi dhaifu la Mobutu ambalo askari wake hawakuwa na mafunzo, vifaa wala mshikamano. 


Aliomba msaada kutoka Ufaransa ambao walimsaidia kwa kuleta Askari wa Morroco wa kikosi cha komando waliofanikiwa kuwashinda waasi Katanga.

Hata hivyo, mwaka mmoja baada waasi wakashambulia tena, ila mara hii wakiwa na wanajeshi wengi zaidi ya awali. Jeshi la Mobutu halikufanikiwa kuzima jaribio na kwa mara nyingine likashindwa tena, huku askari wake wengi wakichana sare zao, wakitupa bunduki na kukimbia uchi msituni. 


Jimbo la Katanga, pamoja na utajiri wake wote wa madini kama vile almasi lilikuwa mbioni kutangaza uhuru wake, na hamna chochote Mobutu angaliweza kufanya. Kwa mara nyingine aliomba msaada wa kimataifa dhidi ya “wakomunisti”. Ufaransa na Ubelgiji walituma vikosi kuzima uvamizi, huku marekani ikitoa msaada wa vifaa na mbinu na vikozi vamizi vilifurushwa tena mpaka mpakani.

Licha ya changamoto hizo Mobutu aliweza kujenga utajiri wake binafsi, ambao mpaka kufikia mwaka 1984 inasemekana alikuwa na dola za kimarekani 5$ billion.


Mobutu aliyekua na msururu wa majumba ya kifahari dunia nzima, alipenda kusafiri safari za muda mrefu pamoja na kufanya shopping maeneo mbalimbali kama vile Disneyworld huko marekani na Paris, huku idadi kubwa ya watu kwenye msafara wake wakipanda ndege ya kukodi aina ya Boeing 747 na Concorde.


Huku akijilimbikizia mali nchi yake ilifulia, mwaka 1989 Zaire ilishindwa masharti ya mikopo ya Ubelgiji—baada ya Mobutu, familia yake na wapambe wake kuiba kwa miaka mingi bila kusita.


Hazina ya nchi hiyo kwa kifupi iliishiwa pesa kabisa jambo ambalo lilisambaratisha miundombinu ya barabara, madaraja na mambo mengine ya maendeleo kwa kuwa hakukuwa na pesa za kuziendeleza. 


Wafanyakazi wengi wa serikali walilipwa kwa mkupuo kiasi cha kusababisha mfumko wa bei na rushwa iliyoumiza sana vichwa.

Kiwango kikubwa cha wizi na ufujaji wa mali za taifa uliofanywa na Mobutu na genge lake dharimu ulisababisha wachumi waite aina ya utawala wake Kleptocracy( Utawala wa wizi).


Hodhi la taswira binafsi ya Mobutu na serikali yake lilitawanyika kila mahali; Picha za Mobutu zilikuwa kila mahali, wafanyakazi serikalini waliamriwa wavae nguo zenye vifungo vyenye picha ya Mobutu, na kwenye TV Mobutu alionekana akishuka kwenye mawingu kama Mesiah. Pia alijiita majina kama “ Mpiganaji dhidi ya simba” “ Mkombozi wa taifa”.


Kuanguka kwa dola ya Sovieti mwaka 1989 haikuwa jambo zuri kwa Mobutu. 


Alikuwa akitegemea sana msaada kutoka magharibi, hata kama walizichukia sera zake za ndani. Kutokana na ukubwa wa kijiografia wa Kongo, hazina kubwa ya madini aliweza kujiweka katika nafasi ya ulinzi dhidi ya tishio la ukomunisti Afrika. 

Na ukweli kwamba nchi yake ilihodhi utajiri mkubwa wa dhahabu, fedha, amasi, mbao n.k hakuwa na shaka. Hata hivyo kwa kuwa Jamhuri ya Urusi haikuwepo tena, madai ya Mobutu kwamba alikuwa ni mpambanaji dhidi ya ukomunisti kwenye moyo wa Afrika hayakuwa na maana tena.

Kutokana na shinikizo la serikali za magharibu na kwa kuwa matatizo ya kiuchumi na migogoro ya ndani, Mobutu aliondoa marufuku ya vyama vya upinzani na kuwakaribisha viongozi wa upinzani kwenye serikali yake.


Licha ya mbinu ya kuwazuga wapinzani kwa lengo la kuwagawanya kwa kuanzisha vikundi pinzani miongoni mwao, chama kikuu cha upinzani kilianzisha taasisi moja mwaka 1994, na kulazimu Mobutu kumteua mmoja wa wanachama wake kama Waziri mkuu. Pamoja na hayo Afya ya Mobutu iliendelea kuzorota , na akaanza kutumia muda mwingi Ulaya kwa matibabu. 


Mwaka 1996 Waasi wa Kitusi wakachukua faida ya kutokuwepo kwake nchini na kufanya uasi uliowawezesha kutwaa himaya ya zaidi ya nusu ya nchi hiyo. 


Waasi wengine wakiongozwa na Laurent Kabila walitwaa Kinshasa mwaka 1997 na muungano wa uasi huo ulilishinda jeshi la Mobutu na kunyakua Kinshasa, Mji mkuu. 

Safari ya ghafla ghafla huku akiwa na gadhabu kwenda uhamishoni iliashiria mwanzo wa hatima ya utawala wake na pengine hata kutoweka kabisa kwenye uwanja wa siasa za Afrika.


Marafiki wa karibu kabisa wa Mobutu walikataa kumpa hifadhi.Togo, taifa lingine la afrika magharibi lililoongozwa na Mdhalimu Gnassingbe Eyadema, lilimwamuru Mobutu na familia yae waondoke siku kadhaa baada ya kuwasili nchini humo wakitokea kongo.


Mobutu akakimbilia uhamishoni Morocco alipokuwa na makazi ya kudumu. Septemba 7 1997 alikufa kwa Kansa ya tezi dume.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: