BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

RAIS DK MAGUFULI ASABABISA ZITTO KABWE WAMTUSI NA KUMDHARAU MKOANI KIGOMA



Ule msemo kuwa ziara za Rais John Magufuli hazijawahi kumuacha mtu salama, ndivyo inavyoweza kufasiriwa kutokana na ujio wake mkoani Kigoma ambao umesababisha kero kubwa kwa Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe anayelalamika kuandamwa kwa matusi na kubezwa katika mitandao ya kijamii.

Anashtumiwa kutokana na uamuzi wake wa kuunga mkono jitihada za Rais Magufuli kuzindua ujenzi wa miradi ya maendeleo.

Akihutubia kwa nyakati tofauti wakazi wa kata za Kasimbu, Kasingirima, Kitongoni, Machinjioni, Rubuga na Kagera zilizopo Tarafa ya Kigoma Kusini, Ujiji mjini Kigoma juzi, Zitto alisema amekuwa akiandamwa na baadhi ya watu wanaotumia mitandao ya kijamii vibaya kwa kumtusi na kumdhalilisha.

Zitto alisema ataendelea kuunga mkono jitihada za Rais kuleta maendeleo mjini hapa kwa vile mkoa upo nyuma kwenye huduma za jamii; barabara, maji, reli, usafirishaji, masoko na uwekezaji.

“Kuna watu mikoa yao kuna barabara hadi kwenye migomba, wana umeme wa uhakika na maji yanapatikana. Sasa sisi tunaposhirikiana na Serikali ili wananchi wetu wapate huduma hizi muhimu za kijamii wanaibuka kutubeza eti tunajipendekeza kwa Serikali,” alisema Zitto na kuongeza:

“Kigoma tulifanya siasa za kiharakati miaka 20 iliyopita na wazee wetu walikamatwa na kukaa Gereza la Bangwe kwa siku 45 wakiwa mahabusu kwa ajili ya kudai haki na demokrasia, ndiyo maana leo hii sisi tunasimama ili kudai maendeleo.”

Aliwataja walioongoza harakati hizo kuwa ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kigoma, Dk Aman Warid Kabourou ambaye wakati huo alikuwa Katibu Mkuu wa Chadema.


Aliyekuwa na Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Kigoma ambaye sasa ni mjumbe wa Kamati Kuu Chama cha ACT, Alhaji Jafari Kasisiko na Makamu Mwenyekiti wa ACT Tanzania bara, Shaaban Mambo ambaye wakati huo alikuwa Katibu Mwenezi Chadema Mkoa wa Kigoma.

Baadhi ya vijana mjini Kigoma walikamatwa na polisi na kupelekwa katika mahabusu kwenye magereza ya Bangwe, Ilagala na Kwitanga kutokana na tuhuma za kufanya vurugu za kisiasa.

Wakati akilalamika kubezwa na kutukanwa, Zitto alisema Rais Magufuli alipotembelea mkoani Kagera baada ya kutokea tetemeko la ardhi Mbunge wa Bukoba Mjini, Wilfred Lwakatare aliomba msaada serikalini kwa ajili ya waathirika.

“Rais alitembelea jimboni kwa Joshua Nasari hatukuona akisema Serikali isipeleke miradi ya maendeleo, bali (Nasari) aliomba isaidie kutatua changamoto zinazowakabili wananchi. Kama huko kote wabunge walikuwa sahihi kuomba msaada kuna tatizo gani kwangu kuomba Serikali itatue changamoto?” alihoji. 


Awali, Diwani wa Mwanga Kaskazini, Clayton Chipando (ACT Wazalendo) alisema watamuunga mkono Rais kila anapoleta miradi ya maendeleo, huku mwenzake wa Kibirizi, Yunus Ruhomvya akisema Manispaa ya Kigoma Ujiji inaendelea kuboresha huduma za afya na kwamba, wazee 11,000 wanatarajia kupata bima ya afya ifikapo 2020.Mwananchi
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: