BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

WAFANYABIASHARA WA WILAYA YA MAFIA, WAZIFANYIA UHUNI MASHINE ZA EFD’S


NI Uhuni. Ndivyo unavyoweza kuelezea baada ya baadhi ya watu kuzichezea mashine za kielektroniki za kutolea risiti (EFD’s) na kusababisha mapato kupotea.

Kutokana na hilo, Serikali imewataka wafanyabiashara kuacha kuzitumia mashine hizo ambazo zimegundulika kuchezewa na kununua nyingine mpya ndani ya mwezi mmoja.

Kwa mujibu wa barua iliyosainiwa na mmoja wa Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), F.S Kayambo kwenda kwa wafanyabiashara wanaotumia mashine hizo, alisema zipo mashine ambazo watu wasio na nia nzuri wamegundua namna ya kuzichezea.

Alisema watu hao huzichezea mashine hizo ili kufifisha mauzo yaliyofanyika jambo linalosababisha kupotea kwa mapato.

Katika barua hiyo Kayambo alitaja aina za mashine ambazo zinachezewa kuwa ni pamoja na Incotex 180, Incotex 131, Incotex 500, Incotex 3005.

Nyingine ni GPRS Punto, Kube, J one, onda RCH Flee, Rch Globe, RCH Bee, DP 500, DP 50, DP 55, MP 55, FP 2000, Checknocrats, Supremo-ETR, Globe Fiscal Printer, Bee ETR, Flea ETR.

Alisema ili kuepukana na tatizo hilo Serikali imeamua mashine hizo ziondolewe kwenye matumizi mara moja.

“Katika kutekeleza jukumu hilo, Serikali imetoa muda wa mwezi mmoja kwa wale wenye mashine hizo kuacha kuzitumia na kununua nyingine.

“Baada ya Septemba 9, mwaka huu, mashine hizo zitafungwa na hivyo kutoweza kutumika. Yule ambaye hatakuwa hajanunua mashine mpya kufikia muda huo hataruhusiwa kufanya biashara vinginevyo sheria itachukua mkondo wake.

“Kama ulivyoitikia wito wa hapo mwanzo tunaamini utaendeleza ushirikiano huu kwa kununua mashine mpya na kuanza kuitumia ndani ya muda uliopangwa,”alisema Kayambo.

Kutokana na hilo, gazeti hili lilimtafuta Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo ili kupata ufafanuzi wa suala hilo kwa kina, ambapo alisema atalizungumzia wiki ijayo.

Gazeti hili lilizungumza na mmoja wa maofisa wa TRA ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema walichugundua ni kwamba baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakipeleka ripoti zenye mauzo machache.

“Baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa si waaminifu kutokana na kuwa wamekuwa wakifanya biashara zao kama kawaida lakini wakati wa kutuma ripoti zao za mauzo ya siku hutuma yanayoonesha mauzo machache.

“TRA baada ya kupokea ripoti hiyo huilinganisha na ripoti halisi ambayo huhifadhiwa na wakala ambaye alimuuzia mashine ya EFD mfanyabiashara ili kubaini kama kuna ukwepaji wowote wa kodi,” alisema.

Alipoulizwa kuhusu bei za mashine hizo na kwamba wafanyabiashara wote wataweza kununua ndani ya mwezi mmoja, alisema. “Mashine zinauzwa kuanzia Sh 700,000 hadi milioni mbili…wataweza kununua kwa sababu awali wengi wao walikuwa hawana lakini baada ya kubanwa walinunua wote,” alisema.

Hatua hiyo imekuja ikiwa imepita wiki kadhaa sasa tangu TRA ilipoanza kuvifungia baadhi ya vituo vya mafuta nchini kutokana na kuuza bidhaa hiyo bila kuwa na EFDs za mamlaka hiyo.

Baadaye Rais Dk. John Magufuli mwenyewe alilizungumzia, huku akitoa siku 14 kwa wamiliki wa vituo vya mafuta nchini kuhakikisha wamefunga mashine hizo na kwamba atakayekiuka agizo hilo atafutiwa leseni yake ya biashara. 


Hata hivyo agizo hilo, liligonga mwamba baada ya mashine hizo kuadimika kwa mawakala.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: