BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

BAADA TU YA KATIBA MPYA KUPITA KWA KUPATA THELUTHI MBILI ZA TANZANIA BARA NA ZANZIBAR, SASA SAMWEL SITTA AVIZIWA MTAANI.


Samuel Sitta.PICHA|MAKTABA.


Dar es Salaam.
Baada ya Bunge la Katiba juzi kufanikiwa kupata theluthi mbili ya wajumbe wa pande zote mbili za Muungano na kupitisha Katiba inayopendekezwa, sasa msuguano kuhusu Katiba unaonekana kuhamia uraiani.



Msuguano kuhusu Katiba hiyo unatarajiwa kuendelea mitaani, ndani ya vyama vya siasa na kwenye majukwaa kutokana na tofauti ya mitizamo iliyoibuka kuhusu Rasimu ya Katiba iliyopitishwa.


Ingawa matokeo ya kura za ushindi yalipokewa kwa furaha na wajumbe waliokuwapo bungeni kwa kucheza na kurusha vijembe kwa wapinzani, huenda kibarua kitakuwa kigumu kwa CCM itakapolazimika kupambana na wananchi, wanasiasa, wanaharakati na viongozi wa dini ‘waliojeruhiwa’ na mwenendo wa Bunge.


Bunge hilo liliendeshwa kwa upinzani mkali kutoka kwa makundi mbalimbali ya watu waliokuwa wakitaka lisimamishwe kwa madai kuwa limechakachua maoni yao kama yalivyopendekezwa kwenye Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni na Tume ya Jaji Joseph Warioba.


CCM na Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar
CCM iliingia doa baada ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Othman Masoud Othman kuzua kizaazaa bungeni Jumatano wiki iliyopita kwa kupiga kura ya hapana katika ibara 22 kwenye Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa.


Mwanasheria huyo ambaye awali alijiondoa kwenye Kamati ya Uandishi kwa kutoridhishwa na mambo yalivyokuwa yanakwenda, alizomewa na baadhi ya wajumbe na kulazimika kutolewa ukumbini akiwa chini ya ulinzi wa askari wa Bunge.


Akizungumza na gazeti hili, Othman alisema kuwa alichofanya kilikuwa ni utashi wake kwa kuwa Serikali ilitamka kwenye Baraza la Wawakilishi na hata nje ya Baraza kuwa haikuwa na msimamo.


“Kwa hiyo kama Serikali haikuwa na msimamo kwa maana ya upande, maana yake ni ipi pengine unisadie… nilipiga kura kwa kuzingatia utashi wangu na maoni yangu,” alinukuliwa Othman.


Ingawa Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, Samuel Sitta alimtetea Othmani kwa kusema wajumbe hawakupiga kura kwa kutumia vyeo vyao, kwa namna wajumbe walivyoonyesha jazba imeonyesha kuwa CCM itapaswa kusafishwa taswira iliyochafuka.


Sitta na viongozi wa dini
Kwa upande mwingine, Sitta amejikuta akiingia kwenye ‘vita’ na viongozi wa dini, baada ya kuwataka waumini wa madhehebu mbalimbali kuupuza nyaraka zilizotolewa na viongozi hao kwa kuwa hazina utukufu wowote wa Mwenyezi Mungu.


Sitta alisema baadhi ya viongozi wa dini wanalenga kuliingiza taifa kwenye machafuko na kwamba yeye hatakuwa tayari kuvumilia hali hiyo.


Waraka huo ulitolewa kwa pamoja na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (FPCT) na Kanisa la Waadventista Wasabato (SDA).


Huku akiwa na waraka huo mkononi, Sitta alisema kuwa lugha iliyotumika haina staha na haikupaswa kutumiwa na watu wanaohubiri dini duniani.


Akizungumzia kauli ya Sitta, Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Methodius Kilaini alisema kauli ya Sitta inaonyesha kuwa amechoshwa na mwenendo wa Bunge la Katiba.


“Sikutarajia kiongozi kama huyo kutoa kauli mbaya kama hiyo kwa Taifa zima. Sikutegemea mheshimiwa kama huyo kusema maneno kama hayo… Huenda ana stress (msongo wa mawazo). Hata ikiwa hivyo, hakupaswa kutoa kauli nzito kama hiyo. Anatakiwa kufahamu kuwa waraka huo umetoka kwa Wakristo wote hapa nchini,” alisema Askofu Kilaini.


Naibu Katibu Mkuu wa Chadema-Bara, John Mnyika jana alisema kitendo cha Sitta na wenzake kushindwa hata kuelewa waraka wa viongozi wa dini na kuuita kuwa “hauna utukufu wa Mungu na wa kipuuzi”, ni wazi wamelewa madaraka wasaidiwe kwa kupumzishwa.


Hata hivyo, jana Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC) Father Raymond Saba, amesema bado wanaendelea kutafakari kauli ya Sitta na kwamba kwa sasa hawajatoa taarifa yoyote.


Akizungumzia kauli ya Sitta, Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Hamad Salim alisema kauli ya kiongozi huyo imeongeza mpasuko wa dini nchini hasa kuhusu mahakama ya kadhi.


“Viongozi wa dini wameipokea kauli ya Serikali kwa kuwa tu alisema ni kiongozi wa Serikali, lakini itatokea shida kama ahadi yao haitatekelezwa,” alisema Salim.


Sitta na Jaji Warioba
Sitta amejikuta kwenye vita ya maneno na Jaji Warioba huku kila mmoja akisisitiza kuwa anafanya kazi aliyotumwa na wananchi.


Akizungumza katika maadhimisho ya miaka 19 tangu kuanzishwa kwa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) hivi karibuni, Jaji Warioba alisema ataingia mitaani kuitetea Rasimu ya Katiba iliyokuwa imebeba maoni ya wananchi.


Alisema kuwa Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba imeondoa mambo manne muhimu.


Hata hivyo, akizungumza jana na gazeti hili alisema kuwa Katiba hiyo imeacha maswali mengi kuliko majibu hasa kwa upande wa Zanzibar.


Sitta alalamikia kutukanwa
Sitta atakuwa na kibarua kingine cha kujisafisha mbele ya wananchi ambao alikaririwa akisema kuwa wamekuwa wakimtumia meseji za matusi za ya 50 kila siku.


Kwa nyakati tofauti wananchi wasiojulikana wamekuwa wakiandika meseji za matusi kwenye mitandano na simu kwa kile wanachosema kuwa Sitta amelazimisha maoni ya CCM yatawale Bunge.


Wananchi wasubiri waelezo zaidi
Baadhi ya wananchi waliohojiwa kuhusu mwenendo wa Bunge hilo, waliwalaumu wajumbe wa Bunge waliokuwa wakisema walipiga kuwa kwa niaba ya wananchi kwenye majimbo yao.


Walihoji ni lini wajumbe hao ambao ni wabunge wao walikwenda kuwauliza iwapo wanataka kupiga kura ya hapana au ndiyo dhidi ya Katiba iliyopendekezwa?


‘Mimi nimesikia tu mbunge wetu (anamtaja) amesema wananchi wake wamechagua kura ya ndiyo. Ni nani alimtuma kwenda kuwa tunataka Katiba hiyo wakati maoni yetu tulitoa tofauti, “ Yohana Change mkazi wa Vwawa, Mbozi.


Mwanaidi Suleiman alisema haelewi nini kilichotokea bungeni, kwa kuwa matarajio aliyokuwa nayo kuhusu Katiba yameyeyuka baada ya kusikia mambo mengi yamekataliwa.


“Nafuu kama wangeondoa mambo mengine, lakini siyo serikali tatu na uraia wa nchi mbili. Mimi hayo niliyaona makubwa sana, kama hayapo sasa Katiba itahusu nini?” alihoji Mwanaidi.


Chadema na wanachama wake.
Hali ya hewa ndani ya Chadema ilichafuka baada ya Sitta kusema kuwa kuna wajumbe wawili wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kutoka Zanzibar walikubali kupiga kura kinyume na msimamo wa vyama vyao.


Sitta alisema kuwa kati ya wajumbe hao, mmoja alikubali kupiga kura na kusema yuko tayari hata kufukuzwa na chama chake.


“Sasa wale wanaotumia mbinu za ovyoovyo ili mchakato huu usikamilike wanapoteza muda, maana ukizuia maji huku, yanaelekea kwenye mkondo mwingine,” alisema Sitta.


Taarifa hizo zilionekana kuwalenga wabunge wa Viti Maalumu, Maryam Msabaha na Mwanamrisho Abama ambao kwa nyakati tofauti walithibitishwa kutafutwa ili apige kura.


“Kweli nimesumbuliwa sana na watu ambao siwezi kuwataja na wananitaka nipige kura na wengine walifika mpaka nyumbani lakini mimi siwezi kushiriki maana nikifanya hivyo dhamiri yangu itanishtaki,” alisema Msabaha.


Naye Abama alisema kuwa alikuwa amepewa ilani na viongozi wake kwamba anatafutwa ili akapige kura, hivyo aliamua kukaa ndani kukwepa mtego huo.


Kauli hizo mbili tofauti zinauachia Ukawa maswali magumu yanayohitaji majibu ili kubaini iwapo kuna usaliti wowote umefanyika au la.


Wabunge wengine ambao wanaweza kukukumbana na matatizo ndani ya chama hicho ni Mbunge John Shibuda (Maswa Mashariki), Said Arfi (Mpanda Mjini) ambao walikiuka uamuzi wa Ukawa kutoshiriki Bunge hilo.


Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa jana alisema kuwa suala la wasaliti wa chama linatarajiwa kuzungumzwa kwenye vikao vya ndani.


“Siwezi kulitolea uamuzi suala hilo, baada ya kumaliza uchanguzi sasa litazungumzwa ndani ya vikao vya chama na kutolewa uamuzi,” alisema Dk Slaa.


Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alisema kuwa Sitta alipaswa kuwataja wajumbe kutoka Ukawa waliokubali kupiga kura, lakini hakufanya hivyo.


“Juzi amechukua kura zao na hawataji ni kina nani wala walipiga kura kwa njia gani. Hata akijiongezea hizo kula mbili feki bado BMK upande wa Zanzibar wanabakiwa na kura 145 tu na siyo 146,” alisema Mtatilo.


Wanananchi waikataa rasimu
Naye Joseph Lyimo kutoka Manyara, amesema kuwa baadhi ya wakazi wa mkoani humo, wamesema Bunge la Katiba limepitisha rasimu ya Katiba bila maridhiano kwa baadhi ya wajumbe hivyo kusababisha hofu ya kupatikana kwa katiba mpya itakayokidhi matakwa ya wananchi.


Wakizungumza jana na mwandishi wa habari hizi, wananchi hao walidai kuwa rasimu hiyo iliyopitishwa bungeni juzi haikukidhi maoni yaliyotolewa kwenye tume ya Warioba kwani ibara 28 zimefutwa na kuwapo ibara mpya 42.


Mkazi wa mji mdogo wa Mirerani, Abdalah Mtengeti alisema kwenye Tume ya Warioba wananchi walipendekeza mbunge awe na ukomo wa madarakani kwa miaka 15, lakini sasa wabunge hao wameridhia asiwe na mwisho wa utawala.


“Wananchi hawawezi tena kumwajibisha mbunge waliyemchagua wao wenyewe kama walivyopendekeza awali pia hakuna ukomo wa mbunge tena hivyo atatawala hadi mwenyewe aseme sigombei tena,” alisema Mtengeti.


Mwenyekiti wa Bavicha Mkoa wa Manyara, Frank Oleleshwa alisema rasimu hiyo ya wabunge haikujali maoni ya wananchi kwani walipendekeza kufutwa kwa vyeo vya wakuu wa mikoa na wilaya lakini, wabunge wameridhia.


“Pia wananchi walipendekeza kuwepo na Serikali tatu ikiwamo kurudisha Tanganyika ili kuwapo na usawa wa nchi, lakini wabunge wamegoma hilo na kuridhia Rais wa Zanzibar awe makamu wa pili wa Rais,” alisema Oleleshwa.


CCM, CUF Zanzibar
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai walipozungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti visiwani humo, Mazrui alisema kwamba mambo yaliyopitishwa na Bunge la Katiba katika rasimu hiyo yanagongana na Katiba ya Zanzibar iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010 ikiwamo suala la mamlaka ya ugawaji mikoa aliyopewa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kushauriana na Rais wa Zanzibar.


Alisema Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano utekelezaji wake utakuwa mgumu kwa baadhi ya mambo Zanzibar mpaka Katiba ya Zanzibar ifanyiwe tena marekebisho na kabla ya kufanyika hivyo lazima kuitishwe kura ya maoni kwa wananchi.


Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema kwamba kama viongozi wote watafanya kazi kwa kuzingatia sheria na katiba, Serikali ya Umoja wa Kitaifa(SUK) haitoyumba kwa sababu hakuna mshindi wala mshindwa baada ya rasimu ya katiba kupitishwa.


“Matokeo ya kura ya rasimu ya katiba, ni ushindi wa wazanzibari wote na watanzania kwa ujumla, na hakuna mshindi wala mshindwa” alisema Vuai ambaye pia alikuwa mjumbe wa bunge maalum la katiba.MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: