BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

YANGA YAANZA LIGI KUU YA VODACOM BAADA YA KUSUASUA KATIKA MECHI MBILI, YAITANDIKA JKT RUVU 4-1.

Kikosi cha kwanza cha Yanga kilichoumana na JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa na kushinda mabao 4-1
 Kikosi cha kwanza cha JKT Ruvu kilichoumana na Yanga kwenye Uwanja wa Taifa na kushinda mabao 4-1.

MABINGWA wa soka Afrika Mashariki na Kati, Yanga, leo wamevuna ushindi wa kwanza tangu kuanza kwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baada ya kuwafunga Maafande wa JKT Ruvu ya Pwani, mabao 4-1 katika mechi iliyochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Wakati ushindi huo ukipeleka faraja kwa mashabiki wa Yanga, kwa upande wa JKT Ruvu ni mwendelezo wa maumivu kwani ni kipigo cha pili mfululizo, ambapo katika mechi iliyopita, walifungwa mabao 2-0 na Simba uwanjani hapo.

Katika mechi hiyo ambayo Yanga ilishuka dimbani bila Kocha Mkuu wake Tom Saintfiet, aliyetimuliwa tangu juzi, wakali hao wa Jangwani walionesha uhai tangu kuanza kwa mechi hiyo.

Yanga wakionesha kiu ya kuondoka na ushindi, ndani ya dakika tatu za kwanza, walifika mara mbili langoni mwa JKT Ruvu kabla ya beki wake, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kuifungia bao la uongozi dakika ya tano, akiunga pasi ndefu ya Athumani Idd Chuji aliyepokea mpira mfupi ya adhabu ndogo ya Harouna Niyonzima.

Baada ya bao hilo, Yanga ikazidi kutawala mchezo na kushambulia mara kwa mara, na kupoteza nafasi kadhaa kupitia wakali wake Simon Msuva na Didier Kavumbagu, waliokuwa mwiba kwa walinzi wa JKT, lakini pia ikikosa kupitia Nizar Khalfan na Hamis Kiiza.

Dakika ya 31, Kavumbagu akaipatia Yanga bao la pili, akiitendea haki pasi ya Oscar Joshua.

Mwamuzi wa mchezo huo Hashimu Abdallah, akamlima kadi ya njano kiungo Ally Khan wa JKT, ambaye alikuwa akijaribu kupunguza kasi ya idara ya kiungo ya Yanga kwa kucheza rafu za mara kwa mara kwa Haruna Niyonzima.

Kavumbagu aliyeonesha uhatari zaidi mbele ya lango kulinganisha na mechi zilizotangulia, aliwachambua mabeki wa JKT Ruvu na kutoa pasi nyoofu kwa Nizar, ambaye alikosa bao kunako dakika ya 35.

Licha ya Yanga kutawala mchezo huo, JKT Ruvu haikuwa nyanya kivile, kwani nayo mara kadhaa ilishambulia na kupoteza nafasi zake, ikiwamo ya Haruna Adolf aliyefumua shuti kali dakika ya 39 na kumbabatiza Kevin Yondani na kuwa koa tasa.

JKT wakarudi tena langoni mwa Yanga dakika ya 43, ambapo shambulizi lao kali likamalizwa na rafu ya Athumani Idd Chuji kwa Adolf na Stanley Mkomolwa aalipiga adhabu ndogo na kukosa. Hadi mapumziko Yanga ikawa mbele kwa mabao 2-0.

Kipindi Yanga ikacharuka zaidi na kufunga mara mbili kupitia kwa Simon Msuva dakika ya 53 na baadaye Kavumbagu tena kunako dakika ya 65.

JKT ikaendelea kupambana, ambapo mtokea benchi Credo Mwaipopo aliyeingia kuchukua nafasi ya Said  Otega, aliifungia bao pekee la kufutia machozi katika dakika ya 65.

Hadi filimbi ya mwisho Yanga ikaibuka na ushindi huo wa mabao 4-1 na kuzika rasmi jinamizi la kufanya vibaya, lililozinduliwa kwa sare ya 0-0 dhidi ya Tanzania Prisons, kisha kichapo cha mbwa mwizi juzi cha mabao 3-0, ilipowafuata Wakata Miwa wa Manungu, kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro.

Huko Chamazi Complex nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam, wenyeji wa uwanja huo, Azam FC, waliibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar, lililowekwa nyavuni mapema kipindi cha kwanza na nyota wa kimataifa wa Ivory Coast, Kipre Tchetche, huku Wakata Miwa hao wakimaliza pungufu.
KWA HISANI YA BLOG:francisdande.blogspot.com
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: